Serikali kuimarisha miundombinu Mara

MARA: Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega, amesema kuwa Serikali itaendelea kujenga na kukamilisha barabara zilizopo mkoani Mara kwa kiwango cha lami.

Hatua hiyo itafungua fursa za kiuchumi na kurahisisha huduma za usafiri na usafirishaji ndani ya mkoa huo na mikoa jirani.

Ulega ameyasema hayo leo, Aprili 18, 2026 alipofungua Kanisa la Waadventista wa Sabato, sambamba na kuongoza harambee ya ujenzi wa shule na zahanati katika eneo la Musati, Wilaya ya Serengeti mkoani humo.

Akizungumza katika hotuba yake, Waziri Ulega ameeleza kuwa Serikali itakamilisha miradi ya barabara inayoendelea, pamoja na kuhakikisha kuwa Uwanja wa Ndege wa Musoma unakamilika na kuanza kutoa huduma za usafiri wa anga.

Amebainisha kuwa hatua hiyo ni utekelezaji wa ahadi na maelekezo ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha Wizara ya Ujenzi inakamilisha miradi yote iliyoanza, inayoendelea, pamoja na ile inayohitaji malipo ya awali ili iweze kukamilika.

“Nitafanya ziara na kukagua miundombinu ya barabara katika Mkoa huu ikiwemo ya Mugumu (Serengeti) kuelekea Musoma Mjini, na pia nitatembelea barabara nyingine ili kujionea maendeleo yake,” amesema Ulega.

Sambamba na hilo, Waziri Ulega amempongeza Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa na Mwenyekiti wa Nyansaho Foundation, Dk Rhimo Nyansaho, kwa kuendelea kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuleta maendeleo kwa jamii, hususan katika sekta za elimu, afya, pamoja na kuwahudumia watu wenye mahitaji maalum kupitia taasisi hiyo.

Kwa upande wake, Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Nyansaho Foundation, Dk Rhimo Nyansaho, amesema kuwa lengo la kuanzishwa kwa Taasisi hiyo ni kuboresha maisha ya jamii kupitia sekta za elimu, afya, na huduma kwa watu wenye mahitaji maalumu.

Amesisitiza kuwa fedha zitakazopatikana kupitia harambee hiyo zitasaidia ujenzi wa shule ya awali na msingi pamoja na zahanati.

Naye, Mkuu wa Mkoa wa Mara, Kanali Evans Mtambi ameishukuru Wizara ya Ujenzi kwa kuendelea kutoa ushirikiano katika Mkoa huo hususan katika suala la ukarabati wa miundombinu pamoja na kutenga fedha kwa ajili ya kuboresha miundombinu hiyo.

Kanali Evans amemueleza Waziri Ulega umuhimu wa kujenga kwa teknolojia ya kisasa barabara ya Arusha – Serengeti ili kuendelea kuchochea fursa za Utalii na kukuza Uchumi katika mkoa huo na Taifa kwa ujumla.

Tukio la ufunguzi wa kanisa hilo limehudhuriwa na mgeni maalum, Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju, Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dk. Rhimo Nyansaho, Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi (CDF) Jenerali Jacob Nkunda, pamoja na viongozi wengine wa Serikali, Chama cha Mapinduzi (CCM), na wananchi wa mkoa wa Mara.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button