Wapigakura Uchaguzi Mkuu juu 26.5%
TUME Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) imetangaza idadi ya wapigakura katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu imeongezeka kwa asilimia 26.53.
INEC imetangaza orodha mpya ya wapigakura na vituo vya kupigia kura vitakavyotumika kupiga kura Oktoba 29, mwaka huu.
Mkurugenzi wa Uchaguzi INEC, Ramadhani Kailima ameeleza katika uchaguzi huo, wapigakura 37,647,235 wameandikishwa Tanzania Bara na Zanzibar.
Taarifa ya Kailima imeeleza idadi hiyo imetokana na mabadiliko ya takwimu za idadi ya wapigakura na vituo vya kupigia kura vitakavyotumika katika Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025 ambayo INEC imepokea kutoka Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC).
“Taarifa hiyo imetolewa baada ya kukamilika rasmi kwa uchakataji wa taarifa za wapigakura waliopo kwenye Daftari la Kudumu la Wapigakura la Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) ambapo idadi ya wapigakura walioandikishwa ni 717,557 na idadi ya vituo vya kupigia kura ni 1,752,” ilisema sehemu ya taarifa hiyo.
Aliongeza kuwa, kutokana na mabadiliko ya takwimu za wapigakura na idadi ya vituo vya kupigia kura yaliyowasilishwa na Tume ya Uchaguzi Zanzibar, idadi ya wapigakura na vituo vya kupigia kura vilivyotangazwa na Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi tarehe 26 Julai, 2025 imebadilika.
Aidha, Kailima alisema mabadiliko hayo yamesababisha jumla ya wapigakura waliopo katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura la Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025 kuwa 37,647,235 badala ya 37,655,559 iliyotangazwa awali.
Katika taarifa hiyo, Kailima alisema idadi hiyo ya wapigakura 37,647,235 ni sawa na ongezeko la asilimia 26.53 kutoka idadi ya wapigakura 29,754,699 waliokuwa kwenye Daftari la Wapiga Kura mwaka 2020.
Kailima alieleza kati ya wapigakura 37,647,235, wapigakura 36,650,932 wapo Tanzania Bara na 996,303 wapo Zanzibar.
Alisema kati ya idadi ya wapigakura 37,647,235, wanawake ni 18,950,801 sawa na asilimia 50.34 na wanaume ni 18,696,439 sawa na asilimia 49.66.
Aidha, taarifa ya Kailima ilieleza pia kuhusu vituo vya kupigia kura, ambapo jumla ya vituo vya kupigia kura vitakavyotumika kwenye Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025 itakuwa ni 99,895.
Alisema kati ya vituo hivyo, 97,348 vipo Tanzania Bara na 2,547 vipo Zanzibar. Idadi hiyo ya vituo 99,895 ni sawa na ongezeko la asilimia 22.47 ya vituo vya kupigia kura 81,567 vilivyotumika katika Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2020.
Sambamba na hayo, alisema kwa mujibu wa kifungu cha 13(1) cha Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani Namba 1 ya Mwaka 2024, uandikishaji wa wapigakura kwa upande wa Zanzibar kwa ajili ya uchaguzi wa rais na wabunge, unazingatia sheria inayohusu uandikishaji wa wapigakura kwa ajili ya uchaguzi katika Baraza la Wawakilishi la Zanzibar pamoja na mabadiliko yatakayofaa.
“Hivyo, Daftari la Wapiga Kura la Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar litakuwa ni sehemu ya Daftari la Wapiga Kura la Tume ya Huru ya Taifa ya Uchaguzi kwa ajili ya uchaguzi wa Rais na Wabunge upande wa Tanzania Zanzibar,” ilisema sehemu ya taarifa hiyo.
Pia, alisema INEC itavipatia vyama vya siasa vinavyoshiriki Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025 orodha ya vituo vya kupigia kura vya INEC vitakavyotumika kwenye Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani wa Mwaka 2025.



