Vijana wahimizwa michezo, utunzaji mazingira

KISARAWE: VIJANA wa Shule ya Sekondari Minaki iliyopo jijini Dar es Salaam, wamehimizwa kushiriki michezo lakini pia kuzingatia upandaji miti na utunzaji mazingira kama sehemu ya mapambano ya mabadiliko ya tabianchi.

Hayo yamesemwa na mashirika mbalimbali yaliyoungana kutumia michezo kama nyenzo ya kuhamasisha utunzaji wa mazingira miongoni mwa wanafunzi nchini kupitia programu ya ‘Play to Zero’, inayotekelezwa na Africa Carbon Agency kwa ushirikiano na wadau wengine wa mazingira.

Kulikuwa na tukio la upandaji miti lililofanyika katika Shule ya Sekondari Minaki juzi, wilayani Kisarawe, likihusisha taasisi kadhaa zikiwemo Switzerland–Tanzania Chamber of Commerce, Jakaya Mrisho Kikwete Foundation (JMKF), Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Halmashauri ya Wilaya ya Kisarawe, na Africa Carbon Agency, wote kwa pamoja wakilenga kukuza ari ya vijana kushiriki katika michezo sambamba na kulinda mazingira.

Mtaalamu wa mazingira kutoka Africa Carbon Agency, Frank Sima, alisema lengo la programu hiyo ni kuhimiza wanafunzi kupenda michezo huku wakijifunza umuhimu wa kupanda na kutunza miti kama sehemu ya mapambano dhidi ya mabadiliko ya tabianchi.

“Tunataka vijana wetu wawe na moyo wa michezo lakini pia wawe na moyo wa kuhifadhi mazingira. Michezo ni jukwaa linalowaleta pamoja na kuamsha ari ya kutenda kwa vitendo,” alisema Sima.

Alifafanua kuwa Play to Zero ilianza mwaka 2023 na imefikia zaidi ya shule 10, ikilenga kuenea kote Tanzania Bara na Visiwani. Aliongeza kuwa programu hiyo inasaidia kuunga mkono kaulimbiu ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan ya kupanda miti milioni 100 kila wilaya nchini.

Kwa upande wake, Mwenyekiti na Mkurugenzi wa Bodi ya Wakurugenzi wa Switzerland–Tanzania Chamber of Commerce, Amne Suedi, alisema ushiriki wao unatokana na imani kuwa elimu ya kuhifadhi mazingira inapaswa kuanza tangu utotoni.

“Tumejumuika hapa na wanafunzi kwa sababu tunataka wajifunze mapema kuwa mazingira ni urithi muhimu. Programu kama Play to Zero ni mfano mzuri wa kuwekeza kwenye kizazi kinachojali mazingira,” alisema Amne.

Kenned Muhoza, Kaimu Afisa Misitu wa Halmashauri ya Wilaya ya Kisarawe, alisema ushirikiano huo ni hatua muhimu katika kupambana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

“Kupitia tukio hili tumeweza kupanda zaidi ya miti 100 kwa kushirikiana na taasisi mbalimbali. Kadiri mabadiliko ya tabianchi yanavyozidi, tunapaswa kupanda miti zaidi,” alisema Muhoza.

Makamu Mkuu wa Shule ya Sekondari Minaki, Kurwa Makene, aliishukuru Africa Carbon Agency na wadau wote waliowezesha mradi huo, akiahidi kuwa shule yake itatunza miti iliyopandwa na kuendeleza kampeni hiyo.

“Tunathamini sana jitihada hizi. Tutahakikisha miti yote inatunzwa na shule yetu inaendelea kuwa mfano bora kwa shule nyingine,” alisema Makene.

Mbali na upandaji miti, wadau hao pia walitoa msaada wa mipira 10 ya michezo, matunda kwa wanafunzi, na filamu ya elimu ya mazingira iliyotazamwa na wanafunzi wa Minaki kama sehemu ya kampeni ya kuunganisha michezo na elimu ya mazingira.

Nahodha wa michezo wa shule hiyo alishukuru taasisi hizo kwa mchango wao, akiahidi wanafunzi wataendelea kuwa mabalozi wa michezo na mazingira katika jamii zao.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button