ACT Wazalendo kudhibiti ufisadi Zanzibar

ZANZIBAR : MGOMBEA urais wa Zanzibar kupitia Chama cha ACT-Wazalendo, Mhe. Othman Masoud Othman, ameahidi kuwa endapo atapewa ridhaa ya kuongoza serikali ya Zanzibar, atahakikisha vitendo vya ufisadi vinakomeshwa kabisa, na kwamba yeyote atakayebainika kujihusisha navyo atachukuliwa hatua kali za kisheria bila upendeleo.

Akizungumza katika mkutano wa kampeni uliofanyika Jimbo la Chumbuni, Othman alisema Zanzibar imechoshwa na wimbi la ubadhirifu wa mali za umma, ambapo kwa miaka mingi baadhi ya viongozi wamegeuza nafasi zao kuwa njia ya kujinufaisha binafsi badala ya kuwatumikia wananchi.

“Zanzibar haiwezi kuendelea kuwa ‘shamba la bibi’. Serikali nitakayoiongoza itasimama imara kuhakikisha mali za umma zinalindwa, na wote waliowahi kuzitumia vibaya watawajibishwa kwa mujibu wa sheria,” alisema Othman.

Amesema katika serikali atakayoongoza, uwajibikaji utakuwa kanuni kuu ya utumishi wa umma, huku akisisitiza kuwa hakuna atakayejificha nyuma ya chama au cheo kuficha uovu.SOMA: Ilani NCCR-Mageuzi, ACT Wazalendo, AAFP na ajenda ya kukuza uchumi

Othman aliongeza kuwa wananchi wamechoshwa na maisha magumu, ukosefu wa ajira na mfumuko wa bei unaoendelea kuwaumiza, hivyo ni wakati wa kutumia kura kuleta mabadiliko ya kweli. “Wazanzibari wamevumilia vya kutosha. Sasa ni wakati wa kusema hapana kwa mateso haya kupitia sanduku la kura, na kuandika historia mpya ya haki, umoja na maendeleo,” alisema.

Alibainisha kuwa Zanzibar ni nchi yenye heshima na utu, hivyo haiwezi tena kuvumilia viongozi wanaopanda madarakani kwa njia zisizo halali. Aidha, Othman alisema umoja wa kitaifa ndio msingi wa maendeleo, akisisitiza kuwa Wazanzibari wakiamua kuweka tofauti zao pembeni, wataweza kujenga Zanzibar mpya yenye maridhiano na ustawi wa kweli.

Hata hivyo, alieleza kuwa bado wapo baadhi ya watu wasiopenda kuona amani ikitawala, wakihubiri kwa maneno lakini wakifanya vitendo vinavyokandamiza haki za wananchi. Ametoa wito kwa vyombo vya dola kuhakikisha vinazingatia wajibu wao wa kulinda raia wakati wa kipindi cha uchaguzi, badala ya kuhusika na vitendo vya unyanyasaji. “Vyombo vya dola vinapaswa kulinda wananchi, si kuwaumiza. Zanzibar mpya tunayoitaka ni ile ya usawa, utu na heshima kwa kila raia,” alisema Othman kwa msisitizo.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button