KIONGOZI wa Upinzani nchini Uganda, Kizza Besigye ,68, amerudishwa gerezani baada ya kuwahishwa hospitali kutokana na afya yake kuzorota kwa njaa kufuatia kugoma kula kwa siku kadhaa akiwa gerezani.
Hatua ya Besigye kugoma kula imetokana na kupinga kukamatwa kwake kwa tuhuma za uhaini na madai ya kutishia usalama wa taifa.
Kupitia ukurasa wa Facebook wa Wakili wake Erias Lukwago, amesema Besigye, alikimbizwa katika kituo cha afya kwa ajili ya matibabu baada ya afya yake kuzorota.
Besigye alishtakiwa katika Mahakama ya Kijeshi kwa makosa ya kumiliki silaha kinyume cha sheria na kutishia usalama wa taifa, ambapo adhabu yake ni kifo, hata hivyo mshtakiwa amekanusha mashtaka hayo.
Mwanasiasa huyu mstaafu, ambaye amewahi kugombea urais dhidi ya Rais Yoweri Museveni mara nne, amekuwa kizuizini tangu alipotekwa nchini Kenya mwezi Novemba na kisha kusafirishwa kurudi Uganda kukabiliana na kesi za mashtaka yanayomkabili.
Chanzo: BBC