BMT yagharamia wachezaji 20 mashindano ya Dunia
BARAZA la Michezo la Taifa (BMT) limegharamia wachezaji 20 wa mchezo wa ngumi na Kabadi kwa ajili ya kuiwakilisha Tanzania katika michuano ya Dunia.
Kati ya wachexzaji hao, watano ni mabondia wa kike wa Timu ya Taifa ya Ngumi za Ridhaa na 15 wa mchezo wa Kabadi.

Taarifa ya baraza hilo iliyotolewa leo Februari 28 imesema Katibu Mtendaji wa BMT Neema Msitha na viongozi wa Chama cha Ngumi za Ridhaa (BFT) na wa mchezo wa Kabadi wamekutana kwa nyakati tofauti kujadili maandalizi ya timu hizo zinazotarajia kwenda Serbia na Uingereza kushiriki mashindano hayo.

Wachezaji watano wa ngumi wanatarajia kuiwakilisha nchi katika mashindano ubingwa wa Dunia wanawake kuanzia Machi 3 hadi 17 katika mji wa Nis , Serbia wakati timu ya Taifa ya mchezo wa Kabadi itaishiriki mashindano ya Kombe la Dunia yatakayofanyika Machi 15 katika jiji la Birmingham, Uingereza.
Msitha amewataka viongozi wa vyama vyote vya michezo vya taifa kuusoma mwongozo wa Serikali wa kuzisaidia timu za taifa.
“Serikali kupitia BMT itazisaidia timu kwa asilimia 25 tu pale inapowezekana huku vyama vyenyewe vikitakiwa kuchangia kwa asilimia 75, hivyo viache kuitegemea serikali peke yake,”amesema.



