BOT: Someni mikataba kuepuka mikopo umiza

WANANCHI wametakiwa kusoma mikataba ya mikopo wanayoenda kukopa kabla ya kukimbilia kusaini na kuangukia kwenye mikopo umiza.

Hayo yamesemwa na Afisa Benki Kuu Tanzania, Mwile Kauzeni alipozungumza na HabariLeo katika Banda la benki hiyo kwenye Maonesho ya 47 ya Kimataifa ya Biashara yanayoendelea Sabasaba

Mwile amesema kuwa wananchi wengi wamekua wakikimbilia kuchukua mikopo kwenye taasisi za kifedha bila kujua taasisi hizo kama zimesajiliwa na BOT au la.

Advertisement

“Wengi  wala hawafuatilii kama hizo taasisi zimesajiliwa na zipo kihalali au la, mbaya zaidi wanasaini bila kuisoma na kuilewa mikataba mwisho wa siku wanaishia kuumizwa kwa kufilisiwa.”Amesema

“Ili mwananchi ajue kama hiyo taasisi ina leseni ya BOT atakuta leseni ya BOT imebandikwa ukutani. Pili aende kwenye ‘website’  ya BOT atakuta orodha ya taasisi za kifedha zilizosajiliwa.” Amesema Mwile na kuongeza

“Akienda huko ajue mkataba wake na hiyo kampuni upoje, wananchi wengi hawasomi mikataba, hawajui ipoje wakipata matatizo wanaanza kulalamika, kwa hiyo waangalie mikataba inasemaje, wajibu wake ni nini? riba watakayochajiwa ni ipi na kama kuna ada nyingine ataiona kwenye mkataba.

“Pia ajaze fomu ambayo itamuonyesha vitu vitakavyokuwepo jina lake, mkopo wa shilingi  ngapi na atalipa kwa muda gani, wahakikishe hivi vyote wamevizingatia kabla ya kukimbilia tu kusaini na kuchukua mkopo.”Amesisitiza

Kauli ya Mwile, imekuja huku kukiwa na wimbi kubwa la wafanyabiashara kulalamikia mikopo umiza iliyopewa majina kama kausha damu na  Kichefuchefu

Wananchi ambao wamekuwa wakichukua mikopo hiyo umiza iwapo wanashindwa kurejesha kwa wakati  wanajikuta wakinyang’anywa mali zao kama viwanja, nyumba, pikipiki, magari, mashamba na kadi za pikipiki na magari zilizokopwa

Hata hivyo, sheria ya biashara ya fedha ‘The Microfinance Act 2018’ inatoa katazo kufanya biashara ya fedha kwa kutoza riba bila kuwa na leseni.

“Kifungu cha 16 cha sheria hiyo kinatoa adhabu kali ya kifungo kisichopungua miaka miwili na kisichozidi miaka mitano kwa anayekiuka sheria hii.

 

 

1 comments

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *