BoT yaonya upotoshaji amana benki za biashara

BENKI Kuu ya Tanzania (BoT) imesema mifumo ya malipo ya Taifa na amana za wateja katika benki za biashara nchini ni salama.

BoT imekanusha taarifa za upotoshaji kuhusu usalama wa mifumo ya malipo na akaunti za amana katika benki na taasisi za fedha nchini.

Taarifa ya Gavana wa BoT, Emmanuel Tutuba imeeleza taarifa hizo zinahamasisha wateja wenye amana kwenye benki za biashara waondoe fedha zao.

SOMA: BoT yatoa hakikisho usalama mifumo ya malipo

Tutuba ameueleza umma taarifa hizo zinaeleza mifumo ya benki itashambuliwa na wahalifu wa kimtandao hivyo kusababisha upotevu wa fedha za wateja na kutopatikana kwa huduma za kibenki.

“Wananchi wanashauriwa kuendelea kutunza amana zao katika benki kwani kuna manufaa mengi yakiwemo fedha kuongezeka kutokana na malipo ya riba au faida ya mwaka, fedha kutunzwa kwa usalama, na uwepo wa bima ya amana endapo benki itafilisika,” alieleza.

Aliongeza: “Amana za wateja zinawezesha benki kutoa mikopo kwa wananchi wanaohitaji mitaji, hivyo kuchangia kukuza Uchumi wa mtu mmoja mmoja na uchumi wa Taifa kwa ujumla.”

BoT imeonya wote wanaosambaza taarifa hizo mitandaoni waache mara moja.

“Tabia hiyo haina tija katika maendeleo ya sekta ya fedha, uchumi wa mtu mmoja mmoja au uchumi wa taifa kwa ujumla,” alieleza Tutuba.

Aliongeza: “Benki Kuu kwa kushirikiana na vyombo vya sheria itachukua hatua kali za kisheria dhidi ya mtu yeyote atakayeendelea kueneza taarifa hizi za upotoshaji.”

Juzi Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa alisema taarifa za upotoshaji kwenye vyombo vya habari ikiwemo mitandao ya kijamii zinalenga kuharibu uchumi wa Tanzania.

“Wanataka kuharibu biashara zetu, wanataka kupunguza watalii ili tukose fedha na kibaya zaidi ni kutaka Tanzania iadhirike ili washindani wetu wa kibishara wanufaike,” alisema Msigwa alipozungumza na waandishi wa habari, Dar es Salaam.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button