CCM kusukuma ujenzi wa barabara Kilolo ~ Moro

IRINGA: CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kimesema kitaendelea kusukuma utekelezaji wa ujenzi wa kipande kilichosalia cha barabara ya lami katika Wilaya ya Kilolo kupitia Kidabala- Boma la Ng’ombe – Morogoro.

Lengo ni kuchochea ukuaji wa uchumi, kurahisisha usafirishaji wa mazao ya wakulima na kuboresha huduma za usafiri kwa wananchi.

Katibu wa NEC Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa CCM Taifa, Kenani Kihongosi amesema hayo leo Juni 19, 2026 aliposhiriki kikao cha wanachama katika Shina Namba Saba Kata ya Mtitu, Kilolo mkoani Iringa.

Kihongosi amesema viongozi wa CCM kwa kushirikiana na wabunge wa Mkoa wa Iringa wataendelea kuishauri Serikali kuhakikisha barabara hiyo inakamilika kwa manufaa ya wananchi wa Kilolo na maeneo jirani.

“Na kwa kuwa na sisi ni viongozi wa kushauri, tutakwenda kushauri hili kazi ikamilike, na kazi hii ikikamilika maana yake itakwenda kuchochea uchumi wa wilaya yetu ya Kilolo. Wakulima watasafirisha mazao, uchumi wa familia utakuwa, uchumi wa wilaya utakuwa na pato la taifa litakuwa,”amesema.

Amesema barabara hiyo ina umuhimu wa kiuchumi na kimkakati kutokana na uwezo wake wa kutumika kama njia mbadala ya usafiri endapo kutatokea changamoto katika eneo la Kitonga.

“Kwa sababu hii njia tunajua inatokezea mpaka Morogoro, lakini pia kama Kitonga ikiharibika, maana yake njia hii inaweza ikatumika kama mbadala. Tutashirikiana kwa pamoja ili kuweza kuiomba Serikali hiyo kazi ikamilike,” amesema Kihongosi.

Amesisitiza kuwa wananchi wa Kilolo wanapaswa kuendelea kushikamana na kulinda utulivu uliopo ili kuweka mazingira mazuri ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika wilaya hiyo.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button