Dk Mwinyi mgeni rasmi Siku ya Kupinga Rushwa Afrika

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk Hussein Ali Mwinyi, anatarajia kuzindua maadhimisho ya Siku ya Kupambana na Rushwa Afrika ambayo yatafanyika mkoani Arusha kuanzia Julai 9-11 mwaka huu.
Akizungumza n waandishi wa habari ofisini kwake, Mkuu wa Mkoa wa Arusha, John Mongella amesema siku ya Mapambano dhidi ya Rushwa Barani Afrika,huadhimishwa Julai 11 kila mwaka, ambapo Tanzania imepewa kuwa mwenyeji wa maadhimisho hayo mwaka huu.
Amesema lengo la maadhimisho hayo ni kutoa nafasi kwa nchi wanachama kutafakari juhudi za mapambano dhidi ya rushwa na kuchukua hatua stahiki kuboresha na kuimarisha mapambano hayo.
“Julai 9 mwaka huu maadhimisho haya yatazinduliwa na Rais Mwinyi kwa kuanza na matembezi ya kupinga rushwa ambayo yataanzia Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Arusha na kuishia Kituo cha mikutano cha kimataifa Arusha (AICC),” amesema.
Amesema maadhimisho hayo yatafungwa Julai 11, ambapo mgeni rasmi atakuwa Rais Samia Suluhu Hassan.