Dkt. Dugange: Toeni fedha za afua za lishe

Naibu Waziri Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Dkt. Festo Dugange
NAIBU Waziri Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa(TAMISEMI) Dkt. Festo Dugange amewaagiza Wakurugenzi wa Halmashauri zote Nchini kuhakikisha wanatoa fedha zote zilizotengwa kwa ajili ya utekelezaji wa afua za lishe kama zilizopangwa katika bajeti.
Akifungua Mkutano wa mwaka kwa maafisa lishe wa mikoa na halmashauri nchini leo Jijini Dodoma Dkt. Dugange amewataka wakurugenzi hao kuhakikisha fedha hizo zinatumika kutekeleza shughuli za lishe na kuacha tabia ya kuelekeza fedha hizo kufanya miradi mingine.
“Baadhi ya wakurugenzi wamekuwa na tabia ya kupeleka fedha za utekelezaji wa afua za lishe kwenye matumizi mengine hivyo ni maelekezo ya Serikali kuhakikisha fedha zote zilizotengwa kwenye bajeti kwa ajili ya utekelezaji wa afua za lishe zinatumika katika afua hiyo na si vinginevyo” amesisitiza Dkt. Dugange.
Amesema Ofisi ya Rais TAMISEMI itafanya tathmini katika Halmashauri zote zilizotenga fedha kwa ajili ya utekelezaji wa afua za lishe, ikibaini fedha hizo kutumika nje ya utekelezaji huo haitasita kuwachukulia hatua wakurugenzi hao.
Vilevile, amewataka Maafisa lishe nchini kuhakikisha wanaimarisha elimu ya lishe kwa jamii kwa kutoa elimu kwa wananchi kuhusu lishe bora kulingana na makundi ya vyakula hasa kwa mama wajawazito, watoto na vijana balee ili kujenga utamaduni wa kutambua umuhimu wa vyakula hivyo.
Pia, Dkt Dugange amewataka maafisa hao kuhakikisha wanasimamia miradi ya afua za lishe kupitia halmashauri zao ili kufikia malengo yaliyokusudiwa na Serikali ya kupunguza changamoto ya lishe nchini.
Aidha, amewataka kuhakikisha takwimu zinazokusanywa kwenye vituo vya kutolea huduma za afya ngazi ya jamii ni sahihi na zenye ubora ili ziweze kutumika kufanya maamuzi katika ngazi mbalimbali.
Serikali kwa kushirikiana na wadau imeandaa na kuzindua Mpango Jumuishi wa Pili wa Taifa wa masuala ya Lishe.
Mpango huo umeandaliwa ili kutoa muongozo kwa wadau wote katika ngazi na nafasi mbalimbali kuhusu utekelezaji wa afua zinazolenga kutatua changamoto za lishe duni (utapiamlo) zinazoathiri watu wa rika zote katika jamii ya Watanzania.
Mpango huo unatekelezwa kwa kipindi cha miaka mitano yaani 2021/22 hadi 2025/26.