DStv, SuperSport Kurusha ‘Live’ Mechi Zote 104 za Kombe la Dunia 2026

DAR ES SALAAM: KAMPUNI ya matangazo ya michezo ya SuperSport kwa kushirikiana na DStv imetangaza kuwa itarusha mubashara mechi zote 104 za FIFA World Cup 2026, mashindano yatakayofanyika katika nchi za Mexico, Canada na Marekani.
Tangazo hilo limetolewa na kampuni hiyo, ambayo ni tanzu ya MultiChoice Group chini ya CANAL+, ikieleza kuwa hatua hiyo inalenga kuwapa watazamaji barani Afrika fursa ya kushuhudia moja kwa moja mashindano hayo makubwa zaidi katika historia ya soka.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, kwa mara ya kwanza wateja wote wa DStv kuanzia kifurushi cha Access hadi Premium wataweza kufuatilia mechi zote mubashara, pamoja na vipindi vya muhtasari na marudio, hatua inayopanua upatikanaji wa mashindano hayo kwa hadhira kubwa zaidi.
Michuano ya Kombe la Dunia 2026 imepanuliwa kutoka mataifa 32 hadi 48 na inatarajiwa kuanza Juni 11, 2026 jijini Mexico City na kuhitimishwa Julai 19, 2026 katika jiji la New Jersey, ikiwa ni toleo lenye mechi nyingi zaidi kuwahi kufanyika.
Katika kuonesha uzito wa tukio hilo, Idris Elba alishiriki kutangaza kuwa mechi zote 104 zitarushwa mubashara kupitia DStv, akiwakilisha uhusiano wa Afrika na jukwaa hilo la kimataifa.
Kwa upande wa bara la Afrika, jumla ya mataifa 10 yamefuzu kushiriki mashindano hayo kupitia Shirikisho la Soka Afrika (CAF), likiwa ni idadi kubwa zaidi kuwahi kutokea. Mataifa hayo ni pamoja na Ghana, Senegal, Morocco, Misri na Afrika Kusini, miongoni mwa mengine.
Akizungumza kuhusu maandalizi hayo, Mkurugenzi wa CANAL+ anayehusika na maudhui na michezo katika Afrika inayozungumza Kiingereza na Kireno, Rendani Ramovha, amesema kampuni hiyo inalenga kuleta uzoefu wa hali ya juu wa utazamaji kwa Waafrika.
Amesema kuwa ushiriki mkubwa wa mataifa ya Afrika unaongeza mvuto wa mashindano hayo, huku akibainisha kuwa vipindi maalum vya uchambuzi na maudhui yatakayozingatia tamaduni za Kiafrika vitaandaliwa ili kuboresha uzoefu wa watazamaji.
Huduma ya matangazo ya Kombe la Dunia 2026 kupitia SuperSport itapatikana katika nchi zaidi ya 25 barani Afrika, ikiwemo Tanzania, Kenya, Nigeria na Afrika Kusini.
Hatua hiyo inatarajiwa kuongeza kwa kiasi kikubwa ushiriki wa watazamaji wa Afrika katika mashindano hayo, pamoja na kuimarisha nafasi ya SuperSport kama mtangazaji kinara wa michezo barani Afrika.



