MKAZI wa Kijiji cha Wangutwa wilayani Wanging`ombe mkoani Njombe, Yuda Nyang`oya (30) amehukumiwa kifungo cha maisha jela baada ya kukutwa na hatia ya kumlawiti mtoto wa kiume mwenye miaka mitano.
Mbele ya Hakimu mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Wanging`ombe, James Muhoni, Mwendesha Mashtaka Mkaguzi Msaidizi wa Polisi, Abraham Kamwela aliileza mahakama kuwa mshatakiwa alitenda tukio hilo Februari 9, mwaka huu.
Mahakama ilielezwa kuwa siku ya tukio alimchukua mtoto huyo ambaye walikuwa wanaishi pamoja katika nyumba ya kupanga na kwenda naye msituni kuwinda kitoweo cha ndege.
Ilielezwa kuwa walipofika msituni mshtakiwa alipanga njama za kufanya kitendo hicho kwa ahadi ya kumpa ndege kitoweo baada ya kumaliza.
Mshtakiwa alifanikiwa kutekeleza ulawiti kwa mtoto huyo.
Ilielezwa kuwa baada ya kitendo hicho, mtoto huyo alirudi nyumbani akiwa na maumivu makali kitu kilichomfanya kumwambia bibi yake ambaye alimkagua na kushudia madhila aliyokumbwa nayo.
Mahakama ilielezwa kuwa bibi huyo alifuata taratibu zote ikiwamo kutoa taarifa kwa Jeshi la Polisi ambao walifanikiwa kumkamata mtuhumiwa na kumfikisha mahakamani. Mshatakiwa alikiri kutenda kosa hilo.