Kampuni ya Tanzania yaweka nguvu umeme jua Zambia

KAMPUNI ya Kitanzania, Amsons Group, imeingia makubaliano ya ushirikiano wa kimkakati na kampuni ya Exergy Africa Limited ya Zambia kujenga na kupanua miradi ya uzalishaji na miundombinu ya nishati nchini humo.

Uwekezaji huo mkubwa nchini Zambia umefanyika kupitia makubaliano ya kujenga na kupanua miradi ya uzalishaji wa umeme wa jua na makaa ya mawe yenye thamani ya jumla ya Dola milioni 900.

Kati ya kiasi hicho, Dola milioni 600 zitaelekezwa kwenye ujenzi wa mradi mkubwa wa umeme wa jua wenye uwezo wa 1,000 MW (1 GW), huku Dola milioni 300 zikielekezwa kwenye uzalishaji wa umeme wa makaa ya mawe wenye uwezo wa 300 MW.

Makubaliano hayo yamesainiwa kupitia ushirikiano kati ya Amsons Group na kampuni ya Exergy Africa Limited ya Zambia, chini ya muunganiko wa wawekezaji wa nishati jadidifu—Africa Power Generation.

Hafla ya utiaji saini ilifanyika Ikulu ya Zambia, ikishuhudiwa na Rais Hakainde Hichilema, ambaye aliusifu mradi huo kuwa hatua muhimu katika kuongeza usalama na utofauti wa vyanzo vya nishati nchini humo.

Rais Hichilema alisema mradi huo wa gigawati moja ni hatua muhimu kwa Zambia, kwani utaongeza upatikanaji wa umeme safi na kutatua changamoto ya mgawo ambayo imekuwa ikichochewa na upungufu wa maji kwenye mabwawa.

Mkurugenzi Mtendaji wa Amsons Group, Edha Nahdi, alisema wanafurahia kushirikiana na Zambia katika mradi utakaosaidia kujenga ajira endelevu, kuongeza uwezo wa ndani na kuimarisha miundombinu ya nishati kwa vizazi vijavyo.

Uwekezaji huo unatajwa kuwa miongoni mwa miradi mikubwa zaidi ya FDI kwenye sekta ya nishati Zambia na ukanda wa Kusini mwa Jangwa la Sahara, na unatarajiwa kupunguza utegemezi wa nchi hiyo kwenye umeme wa maji.

Mkurugenzi wa Exergy Africa, Monica Musonda, alisema ushirikiano huo unaonesha kasi ya bara la Afrika katika kuunganisha rasilimali na utaalamu kutatua changamoto za miundombinu kupitia ubia wa kampuni zenye mizizi barani.

Waziri wa Nishati wa Zambia, Makozo Chikote, alibainisha kuwa serikali inaendelea kuvutia uwekezaji wa sekta binafsi ili kuimarisha ushindani, ubunifu na ustahimilivu kwenye sekta ya nishati.

 

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button