Kocha awapa 5 Watanzania kung’ara Kombe la Dunia

UFILIPINO; KOCHA Mkuu wa timu ya taifa ya wanawake ya Tanzania ya mchezo wa Futsal, Curtis Reid, amewapongeza wachezaji wake kwa kufanya vizuri katika mechi dhidi ya New Zealand.
Timu hiyo inayoshiriki fainali za michuano ya kombe la dunia mjini Manila, Ufilipino, jana ilishinda mabao 4-2 dhidi ya New Zealand na kufanya hali kuwa ngumu katika Kundi C kwenye kuamua timu zitakazocheza robo fainali ya michuano hiyo.
Akizungumza mjini hapa leo Novemba 27, Reid alisema timu hiyo ni nzuri kwa taifa, kwani wachezaji wake walifanya vizuri na kufuata maelekezo yote aliyowapatia.

“Najivunia sana wao (wachezaji) wamekuwa wakicheza kwa kupambana sana, tumecheza mechi nyingi za majaribio na faida zake tumeziona,”alisema na kuongeza:
“Kupata ushindi kama hivi ni jitihada za wachezaji na hii inatia moyo sana kwa sababu hii ni mara ya kwanza kwa Tanzania kucheza mchezo huu katika mashindano makubwa kama haya… Futsal inatakiwa kuheshimika maana imetufanya tumecheza kombe la dunia, naishukuru TFF (Shirikisho la Soka Tanzania) chini ya Rais wake Wallace Karia kwa sapoti wanayotupatia,”alisema.

Ushindi wa jana unaifanya Tanzania kushikaa nafasi ya tatu kwenye msimamo ikiwa na pointi 3 sawa na Japan iliyo nafasi ya pili, New Zealand inashika mkia ikiwa haina pointi na Ureno ndio kinara wa kundi hilo la C ikiwa na pointi sita baada ya kushinda mechi mbili.
Ureno sasa inahitaji pointi moja ili kujihakikishia kufuzu robo fainali, huku Tanzania ikihitaji ushindi dhidi ya Japan katika mechi inayotarajiwa kuchezwa kesho kutwa ili kukata tiketi ya robo fainali.

Aidha mchezaji wa Tanzania Mary Siyame yupo kwenye kinyang’anyiro cha kuwania kiatu cha dhahabu kwa kufunga mabao matatu.
Mary anawania nafasi hiyo na Emily wa Brazil, Vane Sotelo wa Hispania, Ana Azevedo wa Ureno, Sara Boutimah wa Italia, Sara Oino wa Japan na Derika Peanpailun wa Thailand wenye mabao matatu kila mmoja, huku Renata Adamatti wa Italia akiongoza mbio hizo kwa kupachika mabao manne.



