MWIGIZAJI nyota wa filamu nchini Elizabeth Michael ‘Lulu’, ameweka wazi kupitia mitandao wake wa kijamii kuwa amepata mtoto wa kike na kulitaja jina lake kuwa ni Gracious.
Lulu na mumewe Francis Ciza ‘Majizzo’ walifunga ndoa Februari 16 mwaka 2021, ambapo tayari wamebarikiwa mtoto wa kiume aitwaye Genesis.
“Ni kwa Neema ya Mungu tumekutana hapa duniana nikiwa kama mzazi wako, yaani mtu nilieaminiwa na Mungu kulitunza Kusudi lake aliloweka ndani yako mpaka pale utakapopata uwezo na fahamu za kuendelea kufanya hivyo wewe mwenyewe….!
“Ningependa ujue neema hii iliyotukutanisha ndio imekuwa kiungo kikuu kwenye maisha yote ya huyu mzazi wako. Neema ya Mungu ilinipitisha palipoonekana hapawezekani kupita.
“Neema ya Mungu ilinipa mwanzo katika nyakati zilizoonekana kama ndio mwisho kwangu. neema imeniwezesha kumiliki vitu ambavyo vilikuwa kama ndoto tu kwenye maisha yangu.
“Neema ya Mungu imeniweka kwenye nafasi ambazo kibinadamu naonekana sikustahili au hata sasa sistahili kuwepo…ila ndo hivyo nipo.
“Neema ya mungu imeniketisha na wakuu mwanangu…ambao sikudhani kama ingewezekana mimi kuwa sehemu yao.
“ Na hayo ni machache tu katika meeengi ila kwa ufupi Neema ya Mungu ndio maisha yangu, hakuna niliyowahi kuyafanya au ninayoyafanya hata leo hii kwa ujanja wangu au akili yangu ya kibinadamu pekee, “ hayo ni baadhi ya maneno aliyoandika Lulu.