Majaliwa: Serikali itaendelea kufanya mageuzi sekta ya kilimo
WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa amesema kuwa Serikali imedhamiria kuendelea kufanya mageuzi katika sekta ya kilimo ili kuhakikisha Tanzania inaendelea kuwa kitovu cha uzalishaji wa chakula katika ukanda wa Afrika Mashariki.
Amesema lengo la Serikali ni kuendelea kuimarisha usalama wa chakula, kupunguza utapiamlo na kuijenga Tanzania yenye wananchi wenye afya bora, nguvu kazi imara na uchumi unaojitegemea.
Majaliwa amesema hayo leo Oktoba 16, 2025 wakati wa kilele cha maadhimisho ya Siku ya Chakula Duniani ambayo Kitaifa yamefanyika mkoani Tanga.
Amesema kuwa Serikali katika kuhakikisha imefanya mageuzi makubwa katika sekta ya kilimo, iliongeza bajeti ya sekta hiyo kutoka sh bilioni 246 mwaka 2020/2021 hadi sh trilioni 1.3 mwaka 2024/2025.
“Matokeo ya jitihada hizi ni dhahiri: uzalishaji wa mazao ya chakula umeongezeka kutoka tani milioni 18 mwaka 2020/2021 hadi tani milioni 22 mwaka 2023/2024, huku kiwango cha utoshelevu wa chakula kikiongezeka kutoka asilimia 114 hadi 128 mwaka 2024/2025” amesema.
Pia, Majaliwa amewahimiza wakulima, wafugaji na wavuvi kuhakikisha kuwa baada ya mavuno wanaongeze thamani ya mazao kupitia usindikaji na ubunifu, badala ya kuuza mazao ghafi.
Kwa Upande wake Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo, Gerald Mweri amesema kuwa kazi kubwa imefanywa na Serikali katika uwekezaji kwenye sekta ya kilimo iliyowezesha kuifanya nchi kuwa na usalama wa kutosha wa Chakula.
Naye Mwakilishi Mkazi wa Umoja wa Mataifa (UN) hapa nchini Suzan Namondo ameipongeza Tanzania kwa hatua kubwa iliyopiga katika masuala ya kilimo pamoja na usalama wa chakula.
“Kupitia uongozi bora na uwekezaji Tanzania imeongeza kiwango cha uzalishaji wa chakula na kuwezesha nchi hii kupiga hatua kubwa katika utoshelevu wa chakula, hii inaonesha namna Tanzania ilivyo mchangiaji mkubwa katika usalama wa chakula Afrika Mashariki,” amesema Namondo.



