SERIKALI ya mkoa wa Morogoro imewataka madiwani na watendaji wa halmashauri ya Mlimba, Wilaya ya Kilombero kuhamasisha wananchi kuzalisha mazao ya kimkakati ili kuongeza mapato yao na ya halmashauri kwa ajili ya kuboresha huduma za kijamii.
Mkuu wa Mkoa huo, Adam Malima amesema hayo wakati wa kikao cha Baraza la Madiwani wa halmshauri kujadili hoja za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kilichofanyika Mlimba.
Hatua hiyo inatokana na wakulima wa zao la kokoa katika halmashauri ya Mlimba kuanza kufaidika baada ya kufanyika mnada wa kwanza wa ununuzi kwa njia ya mtandao uliowaingizia Sh bilioni 1.1.
Katika mnada huo jumla ya kilo 43,750 za kokoa ziliuzwa Sh 25,720 kwa kilo kupitia mfumo wa stakabadhi ghalani unaoratibiwa na Soko la Bidhaa Tanzania (TMX).
“Halmashauri hii ya Mlimba inaweza kujiendesha kwa kokoa tu endapo uzalishaji ukaongezeka maradufu” amesema Malima.
Amesema mapato ya halmashauri yanategemea mazao ya kilimo yakiwemo mpunga, ndizi na kokoa hivyo madiwani na watendaji wana wajibu wa kusimamia maendeleo.