Mapinduzi ya Kodi Tanzania na somo kutoka IMF

TUNAPOANZA mwaka huu wa 2025 matumaini, ni wakati sahihi kutafakari maendeleo ya Tanzania.
Desemba 18, 2024 Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) lilitoa ripoti ya kina iliyobainisha mafanikio ya nchi chini ya Mpango wa Kuongeza Mikopo (ECF) na Mpango wa Ustahimili na Uendelevu (RSF).
Kimsingi, mipango hiyo imekuwa muhimu katika kuleta utulivu wa uchumi nchini Tanzania, kuendeleza maboresho ya fedha na kukuza uwezo wa kukabili changamoto za mabadiliko ya tabianchi. Tangu ilipozinduliwa mwaka 2022, ECF imewezesha kukamilika kwa mapitio manne mwishoni mwa 2024.
RSF iliyoanzishwa katikati ya 2024 inasaidia juhudi hizi kwa kujikita katika uendelevu wa mazingira. Nyenzo hizi kwa pamoja zinawakilisha mkabala wa jumla wa mageuzi ya kiuchumi na maboresho ya kodi kama nguzo inayoweka
msingi imara wa ustahimilivu na ukuaji endelevu.
Kupitia kutolewa kwa ripoti hii na matokeo yake kuelewa kwa kina, tunaelekeza nguvu na umakini wetu katika mapendekezo yaliyotolewa na IMF kwa kuchunguza namna mikakati hii inavyowiana na malengo ya Tanzania na uwezo wake kuleta maboresho yenye tija.
Kuimarisha ukusanyaji mapato
Mara kwa mara IMF imekuwa ikisisitiza umuhimu wa kuimarisha ukusanyaji wa mapato kama nguzo ya utulivu wa kiuchumi na uendelevu wa kifedha Tanzania. Pendekezo kuu linalenga kupanua vyanzo vya kodi jambo ambalo kimsingi, ni muhimu katika kuzalisha njia thabiti zaidi za mapato zinazoweza kutabirika.
IMF inasema hili linaweza kufikiwa kupitia uimarishaji wa hatua za utekelezaji. Kwa kuzingatia utekelezaji huo, Tanzania itahakikisha taasisi zote zinazotozwa kodi sambamba na watu binafsi zinachangia sehemu yao ya haki na kupunguza ukwepaji unaopunguza mapato ya serikali.
IMF pia inapendekeza kupitisha mikakati itakayoongeza ufanisi katika ukusanyaji kodi. Hii inahusisha pia uboreshaji wa mifumo ya usimamizi wa kodi kupitia teknolojia itakayorahisisha mchakato na kupunguza muda na
rasilimali zinazotumika katika ukusanyaji wa kodi.
Aidha, kuboresha huduma kwa walipa kodi ili kurahisisha utekelezaji na kutoa taarifa wazi na zinazoweza kufikiwa, kutasaidia kupunguza mzigo wa usimamizi kwa walipa kodi na kuchochea ulipaji kwa wakati. Kwa pamoja hatua hizo zinalenga kuunda mfumo thabiti zaidi wa kodi ambao si tu unasaidia mahitaji ya sasa ya Tanzania kifedha, bali pia unajenga msingi thabiti kukabili changamoto za kiuchumi kwa siku zijazo.
Kwa kutekeleza mapendekezo haya ya IMF, Tanzania inaweza kuelekea katika mazingira ya usawa na ufanisi zaidi kifedha ambayo ni muhimu katika malengo yake ya maendeleo ya muda mrefu.
Utafiti uliochapishwa Mei 10, 2019 na Bernardin Akitoby na wenzake uitwao, Kifani katika Ukusanyaji Mapato ya Kodi katika Nchi za Kipato cha Chini,” ulilenga namna nchi zenye mapato ya chini zinavyoweza kuimarisha ukusanyaji wa mapato ya kodi kwa ajili ya maendeleo.
Utafiti huu unaonesha namna maboresho ya kodi nchini Burkina Faso mwaka 2009 hadi 2013 kama mfano muhimu
wa utekelezaji wa mapendekezo ya IMF kuboresha wa uhamasishaji mapato.
Katika kipindi hicho, Burkina Faso ilifanya maboresho makubwa ya kodi yaliyorahisisha mfumo wake wa kodi na kupanua wigo wa vyanzo vya kodi hali iliyowezesha kuwapo ongezeko la mapato ya kodi kutoka asilimia 11.9 hadi asilimia 16.8 ya Pato la Taifa.
Maboresho makuu yalihusisha kurahisisha vivutio/motisha za kodi, kupitia upya misamaha ya Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) na kuanzisha kiwango cha kodi ya mapato ya shirika kilichounganishwa na kupunguzwa. Yakiimarishwa na usaidizi wa kiufundi wa IMF, mafanikio katika hatua hizi yanaonesha ufanisi katika kurahisisha
mifumo ya kodi na kuimarisha utekelezaji katika kukuza uwezo wa kifedha.
Hii inasisitiza manufaa yanayoweza kupatikana kupitia maboresho hayo katika nchi nyingine zenye mapato ya chini ili kuongeza ufanisi katika mapato ya kodi.
Kurahisisha misamaha ya kodi
IMF imeweka angalizo kwa Tanzania ikihimiza maboresho ya kimkakati ya misamaha ya kodi ili kuongeza kasi ya ukuaji wa uchumi. Hili si tu suala la kurekebisha namba, bali hasa kuhakikisha kila punguzo la kodi linakuwa mbegu iliyopandwa vyema ikilenga kuvuna faida za kiuchumi.
Hata hivyo, misamaha ya kodi inapaswa kuwa zaidi ya unafuu wa kifedha na badala yake kuwa kichocheo cha maendeleo. Chukulia mfano wa motisha ya kodi katika Ukanda wa Maeneo ya Huru ya Mauzo ya Nje (EPZs) na Maeneo Maalumu yaKiuchumi (SEZs).
Maeneo haya yameundwa kama majukwaa ya kukuza uchumi unaotegemea usafirishaji nje, lakini ni muhimu kuangalia kama kweli yanavutia uwekezaji halisi na kuhamasisha matumizi ya teknolojia, au kama ni njia zilizofichika za kukwepa kodi.
Aidha, sekta ya kilimo inafurahia vivutio mbalimbali vinavyokusudiwa kuongeza tija. Hata hivyo, ni muhimu kuhakikisha manufaa haya hayatekwi na wale walio nje ya eneo la kilimo, na hivyo kupunguza ufanisi. Kadhalika, huenda pia katika vivutio vya uwekezaji kama vile kodi iliyopunguzwa ya mapato ya shirika katika sekta mbalimbali muhimu zikiwamo za madini au utalii.
Je, motisha hizi kweli zinavutia uwekezaji wa muda mrefu ambao si tu kwamba unadumisha biashara tu bali, pia jamii na mifumo ya ikolojia? Pia, kuna picha pana ya msamaha wa Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) hususani katika bidhaa za anasa.
Kurahisisha na kuboresha mambo haya si tu kutarahisisha mfumo wa kodi, bali pia kutaepusha rasilimali za nchi
kama vile fedha za serikali kutumiwa vibaya kwa manufaa ya wachache.
Kupitia kujikita katika maboresho muhimu ikiwa ni pamoja na kurahisisha misamaha na mfumo wa kodi, Tanzania imedhamiria si tu kuongeza mapato yake, bali pia kufanya mapinduzi katika hali yake ya kifedha na kuunda mfumo wa haki na wa ufanisi zaidi.
Huu si tu mkakati wa kujaza Hazina, bali ni hatua muhimu kuelekea kutumia sera bora za kodi ili kukuza matarajio yake ya maendeleo kwa usahihi na ari zaidi. Hii si tu nadharia kwani tafiti nyingi za kimataifa zinaonesha namna maboresho hayo ya kodi kimkakati yanavyoweza kuchochea ukuaji wa uchumi na kuthibitisha namna Tanzania ilivyo katika njia sahihi.
Katika mahojiano, Ashery Mbasha wa Valiant Associates, alielezea namna Mapinduzi ya Rose ya Mwaka 2003 huko
Georgia yalivyofanya maboresho makubwa ya kodi yaliyorahisisha mfumo wa kodi kwa kupunguza idadi ya kodi na kupitisha kiwango cha kodi ya mapato.
Maboresho hayo si tu yameimarisha utekelezaji, bali pia yamepanua wigo wa vyanzo vya kodi na kuchangia ukuaji wa uchumi huku ukijenga mazingira imara zaidi ya kifedha. Aidha, mwaka 2006, Utah ilitoka katika mfumo wa kodi
inayoongezeka na makundi mengi hadi kufikia kiwango sawa cha kodi ya mapato, ukilenga kurahisisha msimbo wa kodi na kuifanya kuwa ya haki zadi.
Maboresho hayo yamethibisha ufanisi hata katika kudorora kwa uchumi yakionesha uthabiti unaoweza kutokana na mabadiliko kama hayo. Katika nchi zinazoendelea kama India na Mexico, maboresho yamelenga kuimarisha usimamizi wa kodi na kuongeza vyanzo vya kodi.
Maboresho hayo yameongeza mapato na kuendeleza ukuaji wa uchumi na hata kuonesha umuhimu wa sera za kodi
zilizoratibiwa sawia zinazoundwa katika muktadha maalumu wa mazingira halisi ya kiuchumi. Kwa pamoja mifano hii inaonesha athari ya maboresho ya kodi yanayotekelezwa vyema katika nyanja mbalimbali za kiuchumi.
Mifano hii inathibitisha kuwa, wakati maelezo mahususi ya maboresho ya kodi yanaweza kutofautiana kwa kiasi kikubwa kutoka nchi moja hadi nyingine, kanuni za msingi za kupunguza utata, kuimarisha usawa na kuchochea utekelezaji zina manufaa makubwa kwa wote.
Utafiti huu unatoa maarifa muhimu kwa mataifa mengine yanayozingatia maboresho kama hayo kuimarisha ukuaji wa uchumi na ustawi wa kifedha.
Maendeleo katika mchakato wa VAT Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) linasisitiza umuhimu wa maendeleo ya teknolojia katika maboresho ya mifumo ya marejesho na ukusanyaji wa Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) nchini Tanzania.
Kwa kuzingatia uwezekano wa kubadilisha usimamizi wa kodi kwa njia otomatiki, IMF husisitiza ujumuishaji wa teknolojia za juu kurahisisha michakato ya VAT. Kimsingi hatua hii hulenga kuongeza ufanisi, kupunguza makosa ya kibinadamu na kuzuia udanganyifu kwa kuhakikisha ukusanyaji wa VAT unafanyika kwa usahihi na kwa wakati.
Ili kuimarisha maendeleo ya kiteknolojia katika mifumo ya VAT, IMF inasisitiza hitaji muhimu la msaada thabiti wa
kisheria. Kwa msingi huo, ni muhimu kwa Tanzania kutengeneza na kusimamia utekelezaji wa sheria mpya inayowezesha ujumuishaji wa mifumo ya kiotomatiki.
Mfumo huu wa kisheria hauna budi kuendana na mbinu bora za kimataifa ili kutoa msingi thabiti wa kisheria ambao si tu kwamba utakuza uvumbuzi wa kiteknolojia, bali pia utalinda haki za walipa kodi na kuongeza uwazi.
Ili kuimarisha masharti ya kutunga sheria, Tanzania inaweza kusimamia kwa ufanisi zaidi shughuli za VAT zitakazowezesha utekelezaji bora wa kanuni na sheria za kodi, kuongezeka kwa uaminifu miongoni mwa walipa kodi na hata kusababisha kuwapo ongezeko kubwa la ukusanyaji wa mapato.
Mkakati huu pia unaimarisha miundo msingi ya kiuchumi katika taifa na kuifanya kuwa imara na thabiti zaidi kama inavyothibitishwa na matokeo chanya yanayoonekana katika mataifa mengine yaliyofanya maboresho kama hayo.
Mshauri wa Masuala ya Kodi aliyepo Dar es Salaam, Kambarage Nyakasaga anasema ulimwenguni kote, mataifa
hutumia mfumo wa kiotomatiki wa VAT na mabadiliko ya kidijiti kuleta mapinduzi katika mifumo ya kodi kwa mafanikio makubwa.
Anasema mfano mzuri ni nchi za Ujerumani na Australia ambazo kuanzishwa kwa mifumo ya kodi iliyojumuishwa ya kompyuta kumerahisisha mchakato wa utozaji kodi na kupunguza gharama na kuimarishwa kwa huduma. Mifumo hii imebadilisha usimamizi wa kodi na kufanya malipo kuwa bora na sahihi zaidi na kuongeza utekelezaji huku ikipunguza kwa kiasi kikubwa mizigo ya usimamizi.
Katika Afrika, utafiti uliofanywa na Jarida la Kimataifa la Mafunzo ya Masoko Mapya, unabainisha kuwa nchini Nigeria, mabadiliko ya kuelekea mfumo wa otomatiki wa VAT yameimarisha usalama na kuruhusu mabadiliko katika malipo ya kodi.
Mabadiliko hayo ni sehemu ya mpango mpana unaohusisha Mfumo Jumuishi wa Usimamizi wa Kodi (ITAS) unaorahisisha taratibu zote za usimamizi wa kodi na kuwezesha kuwapo mchakato ulioboreshwa na wenye ufanisi zaidi katika ukusanyaji wa mapato.
Irene Chaji wa Shule ya Mamlaka ya Kodi nchini Kenya na wenzake wa Chuo Kikuu cha Moi, wanabainisha kuwa safari ya Kenya kuelekea mifumo ya kodi ya kidijiti imeathiri kwa kiasi kikubwa utekelezaji wa kanuni na sheria za VAT miongoni mwa wafanyabiashara.
Kupitia upunguzaji wa gharama na utata katika utekelezaji, mifumo hiyo imeongeza viwango vya utekelezaji na kukuza ufanisi katika ukusanyaji wa kodi. Mfano huu hutumika kama uidhinishaji thabiti kwa mataifa mengine yanayofikiria kwa namna kama hiyo ukibainisha manufaa makubwa na fursa ya mabadiliko kwa kutumia teknolojia za juu za kodi.
Ujumbe wa ziada
Mapendekezo ya IMF hayaoneshi tu mpango wa utekelezaji, bali pia ni changamoto yenye ushawishi mkubwa kutafakari upya mustakabali wa kifedha wa nchi inayopata msukumo mpya kutokana na mafanikio ya mabadiliko katika mataifa mengine huku ikitengeneza njia ya kusonga mbele.
Katika kutafakari uelewa na maarifa haya, zingatia uwezekano wa mabadiliko ambayo mikakati hii inaweza kuleta katika taifa letu. Je, kwa mustakabali wa Tanzania, mfumo wa kodi wenye usawa, ufanisi na uthabiti zaidi unamaanisha nini?
Je, maboresho haya yanawezaje kufungua fursa za ukuaji na ustawi kwa wananchi wote? Kimsingi, kwa pamoja tutafakari namna Tanzania inavyoweza kutekeleza hatua hizi za ujasiri kufafanua upya mwelekeo wake wa kiuchumi.