MITI 10 yenye uwezo wa kutibu magonjwa mbalimbali hapa nchini imepewa kipaumbele katika mkoa wa Shinyanga kwa kuwa inapatikana kwa wingi katika maeneo hayo.
Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Utafiti wa Misitu Tanzania (TAFORI), Revocatus Mushumbusi amemweleza mwandishi wa HabariLeo alipozungumza naye kuhusiana na tafiti mbalimbali zinazofanywa ikiwepo ya miti dawa hiyo.
Mushumbuzi ametaja miti hiyo kwa majina ya kisukuma na magonjwa inayoweza kutibu kuwa ni nengonengo ambayo sehemu zake zinazotumika ni Mzizi,gome na majani.
“Mti huu unatibu Kifafa, maumivu ya tumbo, Kisonono, Kaswende, matatizo ya kupumua na maumivu ya kichwa,” amesema.
Mti mwingine ni Mwatya ama Nkalya ambao sehemu za mti zinazotumika ni Mzizi,gome na majani, hutibu Kifafa, maumivu ya tumbo, mafua na degedege.
Aina nyingine ya mti ni Mlundalunda sehemu za mti zitumikazo ni Mzizi na gome hutibu Maumivu ya tumbo na matatizo ya mkojo.
Aina nyingine ya mti ni Ngemwambula sehemu za mti zitumikazo ni Mzizi,gome na majani hutibu Maumivu ya tumbo, kifua, matatizo ya kupumua na ngiri.
Pia mti aina ya Ningiwe sehemu zinazotumika Mzizi,gome na majani hutibu magonjwa ya Maumivu ya tumbo, kikohozi, msongo wa mawazo,sonona na kuharisha.
Kwa maelezo ya mkurugenzi huyo mti mwingine ni Mondo sehemu zinazotumika ni Mzizi,gome na majani hutibu magonjwa ya Maumivu ya tumbo, kifafa, utasa.
Na miti aina ya msana sehemu za mti zinazotumika ni Mzizi,gome na majani hutibu Maumivu ya tumbo, kuharisha, ukosefu na upungufu wa damu.
Vile vile Kasuku ambao maeneo yanayotumika ni Mzizi,gome na majani hutibu Homa ya mapafu, vidonda vya tumbo, kifua, madonda, malaria, maumivu ya mwili, koo na mafindofindo.
Na mti wa mwisho ni Mzima au Mjimya maeneo yake yanayotumika ni Mzizi,gome na majani hutibu Matatizo ya ini na Maumivu ya tumbo.
Amesema mafanikio yanayotokana na uwepo wa taasisi hiyo ni kuiwezesha miti hiyo ya asili ya dawa kustawi mashambani ili kukuza upatikanaji wake na kuongeza thamani.
“Jitihada za namna ya kuziotesha kwa mbegu na kuzikuza shambani zimefanyika,” amesema.
Amesema taasisi hiyo imekuwa ikitoa ushauri wa kitaalamu kuhusu matumizi ya teknolojia bora na uendelezaji wa maisitu na kusambaza matokeo ya utafiti kwa wadau kwa ajili ya maendeleo endelevu ya misitu na viwanda vya misitu nchini.