Morocco kukopeshwa euro 650mil kuandaa kombe la dunia 2030

MOROCCO : BENKI ya Maendeleo ya Afrika imepanga  kuikopesha Morocco euro milioni 650 ili kuboresha miundombinu ya usafiri wa nchi hiyo kwa ajili ya michuano ya Kombe la Dunia la FIFA mnamo mwaka 2030.

Hayo yameripotiwa na shirika la habari nchini humo la MAP lililomnukuu mkuu wa benki hiyo ya maendeleo.

Rais wa Benki  ya Maendeleo ya Afrika Akin-wumi Adesina amesema mipango ya ufadhili wa kuiboresha miundombinu ya reli na uwanja wa ndege wa Morocco itawekwa kwenye meza ya bodi ya benki hiyo ili kuidhinishwa.

Advertisement

Morocco itakuwa mwenyeji wa Kombe la Dunia la mwaka 2030, pamoja na wenyeji wenza Uhispania na Ureno. Morocco itakuwa nchi ya pili ya Afrika kuandaa michuano ya Kombe la Dunia baada ya Afrika Kusini kufanya hivyo mnamo mwaka 2010.

Nchi hiyo ya Afrika Kaskazini tayari imeanza mipango ya kuboresha barabara na miundombinu ya reli na anga. SOMA:  Saudi Arabia kuandaa kombe la dunia 2034

Pia inanuia kujenga uwanja mkubwa wa michezo katika eneo la Benslimane, karibu na Casablanca pamoja na kuboresha viwanja vyengine sita.