MRADI wa Uwajibikaji katika sekta ya Elimu ya Msingi (AAI) unatarajiwa kutekeleawa Vijiji vya Kasekese na Lugonesi Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika, mkoani Katavi.
Mradi huo utatekelezwa na taasis iisiyo ya kiserikali ya Usevya Development Society (UDESO) kwa kushirikiana na Taasisi ya WAJIBU.
Akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa mradi huo kwa mgeni rasmi, ambaye ni mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Tanganyika, Alson Uisso, Ofisa Mradi, Francis Mlumange amesema mradi huo utaangazia miundombinu katika sekta ya elimu.
Naye Ofisa Ufuatiliaji na tathimini taasisi ya WAJIBU, Tecla Mleleu amesema mradi huo unatekelezwa katika Halmashauri ya Tanganyika kutokana na ripoti iliyotolewa na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ya mwaka 2017, iliyoangazia hali ya miundombinu ya elimu ya msingi ikijumuisha sera ya elimu.
Mleleu amesema ripoti ya CAG ilibainisha katika shule ya msingi Kasekese kuna mrundikano mkubwa wa wanafunzi na katika shule ya msingi Lugonesi kulibainika uchakavu wa madarasa na madawati.
Kwa upande wake mgeni rasmi, Also Uisso ambaye alimwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Tanganyika, Onesmo Buswelu, ameipongeza Taasisi ya UDESO kwa kushirikiana na Taasisi ya WAJIBU kwa kuichagua wilaya hiyo kutekeleza mradi huo na kuwahakikishia ushirikiano wa kutosha, ili kuleta matokeo chanya.
Thamani ya mradi huo ni Sh 85,075,000, ambao utafanyika katika kipindi cha miezi sita.