Mwanamuziki raia wa mali kuongoza Sauti za Busara 2026

DAR ES SALAAM: Mwanamuziki kutoka nchini Mali, Salif Keita, anatarajiwa kutumbuiza katika toleo la 23 la Tamasha la Sauti za Busara litakalofanyika Februari 5-8, 2026 Zanzibar.
Akitambulika kama ‘Sauti ya Dhahabu ya Afrika’ Keita atashiriki kwa mara ya kwanza kwenye tamasha hilo.
Muziki wake umejikita katika mila za waganga wa jadi wa Mali ‘griot’ na unachanganya urithi wa kitamaduni na midundo ya kisasa.
Zaidi ya muziki, Keita amekuwa mtetezi mashuhuri wa watu wenye ualbino, jambo linaloendana na maadili ya kijamii na kitamaduni ya tamasha la Sauti za Busara.
Mkurugenzi wa Tamasha, Journey Ramadhan, alithibitisha ushiriki wa Keita akisema: “Tunajivunia kumkaribisha Salif Keita, gwiji wa muziki ambaye kazi na harakati zake zinaendana na roho ya Sauti za Busara.”
Toleo la mwaka 2026 litawaleta pamoja wasanii kutoka zaidi ya nchi 20, wakijumuisha mitindo mbalimbali kama taarabu, bongo fleva, afrobeat, fusion na jazz.
Baadhi ya wakali watakaotumbuiza ni Ben Pol, Man Fongo, Pilani Bubu, Lindigo, Sousou na Maher Cissoko, Atanda na Afrojazz Messengers, La Carmen Y Su Familia Musical, pamoja na Rajab Suleiman na Kithara.
Mkurugenzi Mtendaji wa Busara Promotions, Lorenz Herrmann, alisema tamasha la mwaka huu linalenga kuongeza fursa za maonyesho kwa wasanii wa ndani na wa kimataifa, kusaidia biashara za ndani na kuimarisha hadhi ya Zanzibar kama kitovu cha utamaduni.
“Tunajivunia kuandaa moja ya majukwaa muhimu zaidi ya muziki na utamaduni barani Afrika, lakini tunajivunia zaidi mchango wake katika uchumi wa ndani. Tunashukuru kwa msaada wa serikali na wadau wote,” alisema Herrmann.
Tamasha la Sauti za Busara hufanyika katika maeneo ya Stone Town na Fumba Town, likijumuisha maonyesho ya muziki, shughuli za kitamaduni, na matukio ya kijamii.



