Mwanza ipo salama uchaguzi mkuu

MWANZA: KAIMU mkuu wa mkoa wa Mwanza Amir Mkalipa ambaye pia ni mkuu wa Wilaya ya Ilemela amewahakikisha kuwa wakazi wa mkoa wa Mwanza kuwa mkoa huo upo salama na tayari kwajili ya Uchaguzi mkuu utakaofanyika Oktoba 29 mwaka.
Mkalipa amesema hayo leo wakati wa Tamasha la Mbio Pole pamoja na kupongeza mafanikio ya sekta ya Afya. Tamasha hilo lilifanyika katika viwanja vya Hospitali ya Rufaa ya mkoa Sekou Toure.
Mkalipa amesema Serikali imejipanga kwa Uchaguzi mkuu na ameahidi uchaguzi utafanyika kwa uhuru na Amani.
“Kama mkoa Tumejipanga kwajili ya zoezi la Uchaguzi na tutashirikiana kwa ukaribu sana na wananchi. Tutakabiliana na yeyote yule atakaefanya vurugu ” amesema.
Amesema Serikali itahakikisha kura zinapigwa na kutangazwa kihalali. Mkalipa ameagiza wakazi wa Mwanza waendele kuhamasishana ili kushiriki kikamilifu katika Uchaguzi Mkuu.

Katika hatua nyingine, Mkalipa amempongeza Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania Dk Samia Suluhu Hassan kwa maboresha ya sekta ya Afya nchini jambo liliopelekea na Hospital ya Rufaa ya mkoa Sekou Toure kuweza kupata majengo mbalimbali ya huduma za Afya na vifaa Tiba.
Naye Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Sekou Toure, Bahati Msaki amemshukuru Rais Samia kwa kuweza kuwapa mashine ya CT-scan kupitia mradi wa usambazaji wa vifaa tiba vya mionzi(ORIO) yenye thamani ya bilioni mbili.
“Tangu tumeanza huduma hii jumla ya wagonjwa 3647 wamepata huduma ya uchunguzi na uwepo wa mashine hiyo umesaidia kupunguza wagonjwa kupewa rufaa ya kwenda kufanya vipimo hospitali ya Bugando,” amesema.




