NCCR -Mageuzi wasisitiza amani ilindwe

DAR ES SALAAM:Chama cha NCCR Mageuzi, kimesema amani na mshikamano ni utajiri mkubwa kuliko dhahabu almasi, hivyo kila Mtanzania ana wajibu kuilinda kwa gharama yoyote bila kujali itikadi za kidini na kisiasa.
Wito huo umetolewa leo Jijini Dar es Salaam na Katibu Mkuu wa NCCR Mageuzi, Dk Evaline Munisi na kusema kuwa utulivu huo haupo kwa bahati mbaya, unatokana na misingi bora ambayo imewekwa na viongozi wa kisiasa.
Amesema wanaosimamia Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa, Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), tangu kampeni zianze hawajasikia matatizo yoyote.
“Kampeni za awamu hii zimekuwa za tofauti na zile zilizopita sababu zinaenda kidiplomasia na tunashinda kwa hoja kila mmoja akinadi ilani ya chama chake hatukusikia tena mgombea kwa mgombea wakigombana au kulumbana haya ni matunda na matokeo ya maelezi ya mlezi wa vyama vya siasa Jaji Francis Mutungi kongole sana kwake,” amesisitiza Dk Eveline.
Sambamba na hayo amebainisha kuwa bado kuna viashiria ambavyo havina tija kwa Taifa, kwani kuna baadhi ya watu wanafanya chokochoko na kusababisha taharuki kwa Watanzania, wanahamasisha kutotii sheria na kupandikiza chuki ili kuyumbisha dola.



