Nchimbi asema Bandari Kwala ni mageuzi kiuchumi

MGOMBEA Mwenza wa Urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dk Emmanuel Nchimbi amesema ujenzi wa Bandari Kavu ya Kwala ni miongoni mwa miradi mikubwa iliyokamilika chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan iliyoleta mabadiliko ya kimtazamo kwa wakazi wa Pwani na Watanzania kwa ujumla.
Amesema mafanikio makubwa yaliyopatikana nchini katika kipindi cha miaka minne na nusu ya uongozi wa Rais Samia ni ushahidi wa kazi kubwa na uongozi wenye dira ulioibadilisha Tanzania kwa kiwango cha kihistoria.

Dk Nchimbi aliyasema hayo wakati akizungumza katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye Uwanja wa Mama Salmin, Mlandizi, mkoani Pwani. SOMA: Samia: Tunamuenzi baba wa Taifa kwa utawala bora
Alisema kukamilika kwa bandari hiyo kumechochea ukuaji wa biashara, ajira na uwekezaji katika ukanda wa Pwani, na kwamba Tanzania sasa inatambulika kimataifa kama kitovu cha biashara kutokana na diplomasia ya uchumi inayoongozwa na Rais Samia.



