NAIBU Waziri Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Deo Ndejembi amewataka waajiri nchini kuongeza ubunifu kwenye Taasisi na Ofisi zao kwa kuvumbua vipaji vipya walivyonavyo watumishi wao.
Ndejembi ametoa wito huo leo kwenye mkutano wake na watumishi wa Halmashauri ya Manispaa ya Kigamboni ikiwa ni siku ya pili ya ziara yake ya kuzungumza na watumishi ndani ya Mkoa wa Dar es Salaam.
Akizungumza katika mkutano huo, Ndejembi ametoa wito kwa waajiri nchini kuwapeleka masomoni kusomea taaluma nyingine watumishi kutoka kwenye kada yenye watumishi wengi ili waje kusaidia kwenye kada yenye uhitaji wa watumishi.
” Nitoe wito pia kwa waajiri kuvumbua vipaji na talanta zingine walizonazo watumishi wao, unakuta muajiri kwenye eneo lake ana wingi wa watumishi kwenye kada ya ualimu, lakini ana uhaba wa maafisa maendeleo ya jamii au maafisa ugavi, kwanini usiwapeleke Shule hawa walimu ili waje kusaidia kwenye kada zenye uhitaji?
Msiwaache watumishi wenu kwenda kusoma bila kushauriana nao, ni haki yao ya msingi kuongeza elimu, lakini kama muajiri ni vema pia ukatoa ushauri kwa Mtumishi wako anapoamua kwenda kusoma, toeni ushauri mzuri kwao wanapoamua kwenda kuongeza elimu basi wakaongeze kwenye kada zenye uhitaji,” Amesema Ndejembi.
Amewataka watumishi wa Halmashauri ya Manispaa ya Kigamboni kuendelea kufanya kazi kwa bidii ili kumuunga mkono Rais Dkt Samia Suluhu Hassan ambaye ameonesha kwa vitendo dhamira yake ya kunyanyua maslahi ya watumishi nchini.
” Niwakikishie kwa dhati kabisa kwamba Rais wetu Dkt Samia Suluhu Hassan ana mapenzi ya dhati mno na watumishi wa umma, ndio maana tokea aingie madarakani ameboresha sana maslahi yenu, hivyo niwasihi nanyi kumuunga mkono kwa kufanya kazi ya kuwatumikia watanzania kwa upendo na uadilifu,” Amesema Naibu Waziri Ndejembi.