NEEC: Wananchi wanapaswa kupata fursa sawa kiuchumi

DAR ES SALAAM: Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (NEEC) limesema wananchi wote wanapaswa kupata fursa sawa za kiuchumi ili kupata mafanikio kwa manufaa yao na taifa.
Wito huo umetolewa Oktoba 11, 2025 na Kaimu Katibu Mtendaji NEEC, Neema Mwakatobe, alipozungumza kwenye semina maalumu kwa waandishi wa habari jijini Dar es Salaam iliyoandaliwa kwa ushirikiano na Chama cha Wafanyakazi wa Vyombo vya Habari (JOWUTA).

Baraza hilo limeanza kutoa mafunzo kwa waandishi wa habari ili kuwajengea uelewa kuhusu majukumu ya NEEC na fursa mbalimbali za kiuchumi zinazopatikana kwa wananchi, hatua inayolenga kuhakikisha taarifa sahihi za uwezeshaji zinawafikia wananchi kote nchini.
“Wananchi hawawezi kuwezeshwa kiuchumi bila taarifa sahihi. Kupitia nyinyi, wananchi wataweza kujua wapi pa kupata msaada wanapokutana na changamoto za kiuchumi, na namna wanavyoweza kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo,” alisema Mwakatobe.
Mwakatobe alibainisha kuwa katika mwaka wa fedha 2024/2025, NEEC imetumia jumla ya Sh trilioni 2.44 kutoa mikopo kwa wanufaika wapatao milioni 18, wanaume wakiwa asilimia 51 na wanawake asilimia 49. Fedha hizi zimetolewa kwa lengo la kuwawezesha wananchi kujikwamua kiuchumi na kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya taifa.

Mkurugenzi wa Huduma za Taasisi wa NEEC, Gwakisa Bapala, alisema tafiti zinaonesha kuwa asilimia 10 pekee ya Watanzania waliokuwa wananufaika moja kwa moja na ukuaji wa uchumi kutokana na changamoto za mitaji, ujuzi, masoko na miundombinu duni.
“Ili wananchi waweze kushiriki kikamilifu katika kilimo, biashara, uvuvi na sekta nyingine, tunapaswa kuweka mazingira rafiki ya kodi, masoko na ujuzi. Hapo ndipo uwezeshaji utakuwa na maana,” alisema Bapala.
Kwa upande wake, Katibu wa Chama cha Wafanyakazi wa Vyombo vya Habari (JOWUTA), Selemani Msuya, aliishukuru NEEC kwa kutoa elimu hiyo muhimu, akisema semina hiyo itawafanya wanachama wake kuwa mabalozi wazuri wa kufikisha taarifa za uwezeshaji kwa wananchi.
Warsha hiyo ilijumuisha mada mbalimbali zikiwemo mifuko na programu za uwezeshaji wananchi kiuchumi, ushiriki wa Watanzania katika uchumi, utoaji wa huduma za biashara, na muongozo wa watoa huduma za biashara.
Kwa mujibu wa NEEC, ushirikiano huu na vyombo vya habari utasaidia kuongeza uelewa wa umma kuhusu fursa za kiuchumi, na kuchochea ushiriki wa wananchi katika kujenga uchumi imara wa taifa.



