Ngajilo ajiita “Moto Ulao”, aapa kukemea ubadhirifu Iringa Mjini

IRINGA: Mgombea ubunge wa Jimbo la Iringa Mjini kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Fadhili Ngajilo, amejiita “moto ulao” akiahidi kuwa, endapo ataaminiwa kuwa mbunge, atashughulika ipasavyo na wote wanaohujumu mali za umma katika maeneo mbalimbali ya jimbo hilo.
Akizungumza katika mkutano wa kampeni uliofanyika kata ya Ilala, Ngajilo alisema amepokea changamoto nyingi kutoka kwa wananchi, ikiwemo ubadhirifu wa miradi ya maendeleo, na kuahidi kushirikiana na madiwani kuhakikisha kila senti ya umma inatumika ipasavyo.
“Ngajilo ni moto ulao. Hapa Ilala kuna eneo linaitwa kamficheni kuna ubadhirifu, tutashughulika. Sambamba na hilo, tutaboresha miundombinu, kuimarisha sekta ya afya, na kusimamia mikopo ya vijana na akinamama ili wajikomboe kiuchumi,” alisema.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa CCM Manispaa ya Iringa, Said Rubeya, aliwataka wananchi kujitokeza kwa wingi kupiga kura akisisitiza kuwa chama hicho kinaelekeza, na wao kazi yao ni kutekeleza.
“Dalili za ushindi ni kubwa, lakini hatutaki ushindi wa maneno. Tunataka watu wengi zaidi wapige kura kwa amani. Amani ni yetu, na Mungu anatupenda kwa sababu tunapenda amani,” alisema.

Rubeya alionya wanaohubiri vurugu kuelekea siku ya kupiga kura kuwa wanapoteza muda, akisema:
“Achaneni na maneno ya kukinukisha, hakuna chochote kitakachotokea. Hizi ni propaganda. Tuhamasishane kushiriki uchaguzi huu kwa amani,” alisema.



