Ngajilo ataka wenye ulemavu wasifichwe suala la elimu

IRINGA; Watoto wenye maisha duni wanaosoma katika shule za msingi mjini Iringa wamepata faraja baada ya Mbunge wa Jimbo la Iringa Mjini, Fadhili Ngajilo, kukabidhi msaada wa vifaa mbalimbali vya elimu na mahitaji muhimu, huku akitoa wito kwa wazazi kuhakikisha kila mtoto, wakiwemo wenye ulemavu, anapata haki ya elimu.
Katika hafla iliyofanyika Shule ya Msingi Ugele, Ngajilo alikabidhi magodoro, madaftari, matranka, pamoja na chakula ikiwemo mahindi na maharage, akisema lengo la msaada huo ni kuboresha mazingira ya kujifunzia na ustawi wa watoto wanaotoka kwenye familia zenye mazingira magumu.

Akizungumza na wazazi, walimu na viongozi waliohudhuria hafla hiyo, Ngajilo alisema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dk Samia Suluhu Hassan imeweka kipaumbele kuhakikisha kila mtoto anapata elimu bila ubaguzi, hivyo hakuna sababu ya kuwaficha watoto wenye ulemavu majumbani.
Alisema watoto hao wana uwezo wa kufikia mafanikio makubwa endapo watapata nafasi ya kusoma na kulelewa katika mazingira yanayowawezesha kutumia vipaji vyao.
“Ninawasihi wazazi msiwafiche watoto wenye ulemavu. Wapelekeni shule kwa sababu huwezi kujua atakuwa nani kesho. Elimu ndiyo ufunguo wa maisha yao na msingi wa mafanikio yao,” alisema Ngajilo.

Alitoa mfano wa watu wengi wenye ulemavu walioweza kufanikiwa katika nyanja mbalimbali za maisha, wakiwemo viongozi na wabunge, akisisitiza kuwa ulemavu si kikwazo cha kufikia ndoto.
Mbunge huyo pia aliwapongeza walimu wanaofundisha watoto wenye mahitaji maalumu kwa kujitolea kwao, akisema kazi wanayoifanya ni ya wito na imeendelea kuwapa watoto hao matumaini ya maisha bora licha ya changamoto wanazokabiliana nazo.
Aidha, aliwataka wazazi kushirikiana kwa karibu na walimu katika malezi na elimu ya watoto wao kwa kufuatilia maendeleo yao ya kitaaluma hata wanaporudi nyumbani, ikiwemo kuwasaidia kufanya kazi za nyumbani (homework), hatua ambayo alisema itachangia kuongeza ufaulu.
Ngajilo alisema uwekezaji katika elimu ni msingi wa maendeleo ya jamii na taifa, akieleza matumaini yake kuwa watoto wanaolelewa na kuelimishwa leo ndiyo watakaokuwa madaktari, wahandisi, walimu, maprofesa na viongozi wa kesho.
Hafla hiyo ilihudhuriwa na viongozi wa serikali, walimu, wazazi na wanafunzi, huku msaada uliotolewa ukitarajiwa kuboresha mazingira ya kujifunzia na kuongeza fursa za watoto wenye maisha duni kupata elimu bora.



