NMB yatoa mabati 400 vituo vya afya Tandahimba

BENKI ya NMB imetoa msaada wa mabati 400 katika vituo viwili vya afya, vilivyopo wilayani Tandahimba uliogharimu Sh 17,200,000.
Msaada huo wa mabati umetolewa katika kituo cha afya kilichopo Kijiji cha Mnyawa, mabati 200 pamoja na kituo cha afya Nachunyu mabati 200.
Meneja wa Benki ya NMB, Kanda ya Kusini, Janeth Shango akikabidhi msaada huo amesema, katika kazi zao wanazofanya changamoto ya sekta ya afya kwao ni kipaumbele, kwa sababu wanaamini mwananchi mwenye afya bora, ndiye anayeweza kufanya maendeleo makubwa na bora zaidi.
Amesema ili jamii iendelee kuwepo, ni lazima iwe na afya nzuri, ambayo inapatikana kutokana na vituo hivyo vya afya, hivyo benki hiyo inashirikiana na serikali kuhakikisha wanaboresha afya za wananchi.
“Tunatambua kabisa juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita katika kusimamia upatikanaji wa afya bora, kuboresha mazingira ya utoaji huduma za afya katika maeneo mbalimbali nchini na tumekuwa tukisaidia pia katika sekta ya elimu na majanga katika Jamii, ” amesema Shango.
Mkuu wa Wilaya ya Tandahimba, Kanali Patrick Sawala ameishukuru NMB kwa kuwa wadau wakubwa wa maendeleo wilayani humo, ambapo imekuwa ikitoa msaada kwenye sekta mbalimbali zikiwemo afya na elimu.