DAR ES SALAAM – KLABU ya Simba imeamua kuachana na kiungo wake mshambuliaji raia wa Burundi, Saido Ntibazonkiza.
Ntibazonkiza alijiunga na wekundu hao wa Msimbazi wakati wa dirisha dogo la usajili mwaka 2022 akitokea Geita aliyoitumikia kwa nusu msimu baada ya kutoka Yanga mwanzoni mwa msimu wa mwaka 2022/23.
Kwa mujibu wa taarifa rasmi kutoka kwenye mtandao wa kijamii wa klabu hiyo jana, mshambuliaji huyo wa kimataifa wa Burundi amemaliza mkataba wake na Simba imeamua kutompa mkataba mpya.
Kiungo huyo mshambuliaji aliyewahi kucheza soka la kulipwa Uholanzi na Ufaransa ameitumikia Simba kwa msimu mmoja na nusu. Akiwa Simba alishinda tuzo ya mfungaji bora sambamba na aliyekuwa mshambuliaji wa Yanga, Fiston Mayele kwa kila mmoja kufunga mabao 17 msimu wa mwaka 2022/23.
SOMA: Rais Samia awasili Pretoria
Aliiongoza Simba kufika mara mbili mfululizo hatua ya robo fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika kabla ya kutolewa na Wydad Casablanca msimu wa mwaka 2022/23 na Al Ahly ya Misri msimu huu.
Ntibazonkiza alishindwa kumaliza msimu wa mwaka 2022/23 na Yanga baada ya kutimuliwa kutokana na matatizo ya kinidhamu kuelekea mchezo wa nusu fainali ya Kombe la Shirikisho la Azam (sasa CRDB) dhidi ya Simba huku akiwa tayari ameshinda ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara.