Papa Francis ahimiza kuwakumbuka maskini

PAPA Francis amewataka waumini kutafakari matumizi makubwa ambayo hufanywa kwenye sherehe za mwisho wa mwaka ikiwemo Krismasi, badala yake wawakumbuke wale wanaoteseka kutokana na vita na umaskini.
Papa alitoa wito huo alipoongoza maombi ya mkesha wa Krismasi katika kanisa la Mtakatifu Petero uliohudhuriwa waumini takribani 7,000.
Papa alisema vita na machafuko mengine yanatokana na uchoyo na tamaa ya madaraka, vitu ambavyo vinasababisha jamii kuangamia.
Kwenye hotuba yake, Papa Francis alionekana kulenga zaidi vita baina ya Ukraine na Urusi.
Hii ilikuwa mara ya kwanza katika miaka miwili tangu janga la Covid-19 kuanza, kwa umati mkubwa wa waumini kuhudhuria misa hiyo ya mkesha wa Krismasi mjini Rome.
Inaelezwa kwamba waumini wengine 4,000 walifuatilia misa hiyo wakiwa nje kwenye viwanja vya kanisa hilo.