Pemba ‘mguu sawa’ ujio wa hoteli mpya ya kifahari

Pemba. Uzinduzi wa NH Collection Pemba Wellness Resort utakaofanyika hivi karibuni unatarajiwa kuleta mapinduzi katika sekta ndogo ya utalii wa kifahari katika visiwa vya Pemba.

Aina hii ya utalii unakuwa kwa kasi hivyo, uwekezaji wa Uzinduzi wa NH Collection Pemba Wellness Resort unatarajiwa kuongeza chachu katika sekta ya utalii na kukuza uchumi wa visiwa hivyo.

Mradi huo unaoendelezwa na Infinity Developments na wenye thamani ya zaidi ya dola milioni 70 za Marekani, ni upanuzi wa uwekezaji wa kampuni hiyo Zanzibar inayozidhi kujipambanua kama mmoja wa wawekezaji wakubwa wa sekta binafsi wanaounda mustakabali visiwani humo.

Mradi huo unaojengwa kwenye mwambao wa Kisiwa cha Pemba unatajwa kuwa kituo cha kimataifa cha ustawi kilichobuniwa kuunganisha ukarimu wa kifahari, huduma za kinga za afya, mazingira ya asili na maisha endelevu katika eneo moja.

Beyond Design, mradi wa NH Collection ni kampuni iliyobuni mradi huo unatarajiwa kuendelea kuimarisha nafasi ya Infinity Developments kama kampuni kubwa na inayoongoza Zanzibar, ikiwa na thamani ya jumla ya maendeleo (GDV) inayozidi dola milioni 600.

Mkurugenzi Mtendaji wa Beyond Design, Karla Seliman, alisema mradi huo umebuniwa ili kuleta muunganiko wa kipekee kati ya maisha ya kifahari, ustawi na mazingira ya asili ya kipekee ya Pemba.

“Maono yetu kwa NH Collection Pemba yalikuwa kubuni eneo la utulivu linalohisi kuunganishwa kwa karibu na mandhari ya kisiwa hiki huku likitoa uzoefu wa hali ya juu wa ukarimu wa kimataifa,” alisema.

“Tulitaka kila kipengele cha usanifu na mapambo ya ndani kuchochea utulivu, ustawi na faragha, huku tukidumisha uhalisia na uzuri wa Pemba. Huu ni mradi ambapo mazingira ya asili, ustawi na usanifu wa kisasa vinaishi kwa maelewano kamili.”

Uzinduzi huo pia unakuja wakati ambapo Pemba imeanza kuvutia tena wawekezaji kufuatia maboresho makubwa ya miundombinu yanayoongozwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, ikiwemo upanuzi wa mtandao wa barabara na ujenzi unaoendelea wa Uwanja wa Ndege wa Pemba.

Wadau wa sekta hiyo wanasema maboresho hayo yanaisaidia Pemba kuwa eneo la utalii lenye ushindani zaidi na linalofikika kwa urahisi, jambo linalofungua milango kwa uwekezaji mkubwa wa kimataifa katika sekta ya ukarimu.

Akizungumza kabla ya ufunguzi rasmi wa mradi huo, Mwenyekiti na Ofisa Mtendaji Mkuu wa Infinity Developments, Samuel Saba, alisema mradi huo unaonyesha kuongezeka kwa imani katika uwezo wa Zanzibar kwenye sekta ya utalii pamoja na dira ya muda mrefu ya maendeleo ya serikali.

SOMA: SMZ, Infinity kushirikiana mradi wa uhifadhi utakaogharimu dola mil 12 

“NH Collection Pemba inawakilisha sura mpya si tu kwa Infinity Developments, bali pia kwa Kisiwa cha Pemba chenyewe,” alisema.

“Tunaona mabadiliko makubwa yanayoendeshwa na uongozi wenye maono, uwekezaji katika miundombinu na mazingira rafiki ya uwekezaji yaliyoanzishwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. Juhudi hizi zinafanya iwezekane kwa miradi ya kimataifa kama huu kustawi.”

Saba alisema mradi huo unaendana na azma pana ya Zanzibar ya kupanua wigo wa bidhaa zake za utalii zaidi ya likizo za kawaida za ufukweni kwa kuvutia wageni wa ustawi na maisha ya kisasa wenye matumizi makubwa.

“Mwelekeo wa utalii duniani unabadilika. Wasafiri wa leo wanatafuta fursa inayozingatia ustawi, uendelevu na uhusiano wa karibu na mazingira ya asili. NH Collection Pemba imebuniwa mahsusi kukidhi mahitaji hayo,” alisema.

Hoteli hiyo ina jumla ya vyumba 171, vikiwemo suites 140, villa moja maalum ya mmiliki yenye bwawa binafsi, villa tano za vyumba viwili vya kulala, villa tatu za msituni za chumba kimoja, villa nane za msituni za vyumba viwili na villa 15 za chumba kimoja, zote zikiwa na mabwawa binafsi.

Kwa mujibu wa waendelezaji, mradi huo unaunganisha anasa za kisasa na mazingira ya asili ya Pemba kupitia usanifu na mandhari yaliyoandaliwa kuleta uzoefu wa utulivu na kuzama kikamilifu katika mazingira ya kisiwa hicho.

Katikati ya hoteli hiyo kutakuwa na kituo kikubwa cha ustawi na afya kinachounganisha ukarimu na huduma za kinga za afya katika eneo moja.

Huduma zitakazopatikana ni pamoja na vyumba vya spa, hammam, sauna, vyumba vya mvuke, jacuzzi, mapango ya chumvi, maeneo ya kuogea maalum na sehemu za mapumziko, sambamba na huduma maalum za ustawi kama cryotherapy, tiba ya oksijeni ya hyperbaric, IV therapy, studio za urekebishaji wa mwili na vyumba vya tiba za urembo.

Mradi huo pia unajumuisha maeneo ya chakula pembezoni mwa bahari, baa ya juu ya jengo, mabwawa ya infinity, vituo vya mazoezi, viwanja vya padel, viwanja vya mpira wa kikapu pamoja na njia maalum za baiskeli na matembezi zilizounganishwa na mandhari ya eneo hilo.

Bw Saba alisema mradi huo umebuniwa kwa makusudi kuiweka Pemba katika ramani ya sekta ya utalii wa ustawi duniani inayokua kwa kasi na inayovutia wageni wa kimataifa wenye matumizi makubwa.

“Hii si hoteli ya kifahari tu. Ni eneo lililojengwa kuzunguka ustawi, maisha marefu na maisha ya kiafya huku likidumisha viwango vya juu vya ukarimu vinavyohusishwa na chapa zinazotambulika kimataifa kama NH Collection,” alisema.

Pia aliipongeza Serikali ya Zanzibar kwa kuunda mazingira mazuri yanayoendelea kuvutia uwekezaji wa kimkakati katika sekta ya utalii na miundombinu.

“Ushirikiano tulioupata kutoka taasisi za serikali umekuwa muhimu sana. Kuna dhamira ya wazi ya kuiweka Zanzibar kama kitovu cha kimataifa cha utalii na uwekezaji chenye ushindani mkubwa, na wawekezaji wanaendelea kuitikia kwa mtazamo huo chanya,” alisema.

Wachambuzi wanasema ujio wa chapa zinazotambulika kimataifa katika sekta ya ukarimu Pemba unaashiria kuongezeka kwa imani ya kimataifa katika sekta ya utalii Zanzibar, ambayo ni moja ya nguzo kuu za uchumi wa visiwa hivyo.

Mbali na utalii, mradi huo unatarajiwa kuunda nafasi za ajira wakati wa ujenzi na uendeshaji, huku ukiunga mkono biashara ndogo ndogo na minyororo ya ugavi ya ndani.

“Kadri upatikanaji wa huduma unavyoimarika na uwekezaji unavyoongezeka, Pemba inaendelea kuwa moja ya maeneo yanayochipukia kwa kasi na yenye kuvutia zaidi katika ukanda huu,” alisema Saba.

“Tunaamini NH Collection Pemba itasaidia kuinua hadhi ya kimataifa ya kisiwa hiki huku ikichangia ukuaji endelevu wa uchumi na maendeleo ya jamii.”

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button