Ripoti: Kenya yazidi kuathiriwa na mihadarati

RIPOTI ya Global Organised Crime Index zinaonesha kuwa Kenya imeendelea kuwa miongoni mwa vituo vikuu vya usafirishaji wa dawa za kulevya, hususan kokeini, katika ukanda wa Afrika Mashariki, licha ya juhudi za nchi za EAC kupambana na biashara hiyo haramu.Hali hiyo imeibua wasiwasi mkubwa kutokana na madhara ya dawa hizo kwa afya ya jamii, usalama na uchumi wa taifa.
Kwa mujibu wa Ripoti ya Idara ya Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI) ya Oktoba 2025, Jiji la Nairobi limegeuka kuwa njia muhimu ya kupitisha dawa za kulevya kimataifa. Ripoti hiyo inaeleza kuwa viwanja vya ndege, ikiwemo JKIA, vinatumiwa na mitandao ya kihalifu kusafirisha mihadarati, jambo linaloathiri taswira ya Kenya kimataifa.
Pia imeeleza wazi kuwa nafasi ya kimkakati ya Nairobi kama kitovu cha usafiri wa anga na nchi kavu imechangia tatizo hilo. Mwaka 2025, polisi wa Kenya walivunja mtandao wa kimataifa wa kokeini uliokuwa ukitumia JKIA na kukamata gramu 750 za dawa hizo.
Mbali na kokeini, Kenya pia inakabiliwa na ongezeko la usafirishaji na matumizi ya heroini na dawa za kisintetiki kama methamphetamine na MDMA, huku Bandari ya Mombasa ikitajwa kuwa lango kuu la kuingiza dawa hizo kwa njia ya bahari.

Utafiti wa NACADA wa mwaka 2022 umebaini kuwa matumizi ya dawa za kulevya yanaathiri uzalishaji wa nguvu kazi na ukuaji wa uchumi. Ingawa Serikali ya Kenya imechukua hatua za kuimarisha mapambano dhidi ya dawa za kulevya, ikiwemo kuimarisha Kitengo cha Kupambana na Mihadarati (ANU), changamoto bado ni kubwa.
Serikali imesisitiza kuwa biashara hiyo imefikia kiwango cha kutisha na inahitaji hatua za haraka na madhubuti kuzuia Kenya kuendelea kuwa kitovu cha dawa za kulevya katika kanda. SOMA: Jinsi Rushwa Inavyodhoofisha Uchumi wa Kenya



