Samia: Chaguzi zitakuwa huru na haki

WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, (Sera, Bunge na Uratibu) William Lukuvi amevihakikisha vyama vyote vya siasa nchini kuwa dhamira ya Rais Samia Suluhu Hassani ni kuhakikisha chaguzi zote zitakazofanyika chini ya utawala wake zitakuwa huru na haki.
Waziri Lukuvi ameyasema hayo  leo jijini Dar es Salaam wakati alipokuwa anafanya ziara kwenye vyama vya siasa kwa lengo la kujitambulisha.

Waziri Lukuvi amesema kwa kutumia 4R za Rais Samia ikiwemo Maridhiano (Reconciliation), Ustahamilivu (Resilience), Mageuzi (Reforms), na Kujenga Upya Taifa (Rebuilding) atahakikisha uchaguzi wa Serikali za Mtaa unakuwa huru na wa haki.

“Nataka niwatoe hofu vyama vyote 19 kuwa kwenye uchaguzi ujao chini ya Rais Samia utakuwa huru na wa haki,” amesema Lukuvi.

Waziri Lukuvi amevitaka vyama vyote vitakavyoshiriki uchaguzi wa Serikali za Mitaa kujiandaa kushindana kwa sera ili wananchi waamue.

Advertisement

Akizungumzia ziara yake hiyo, Waziri Lukuvi amesema ziara  hiyo ni ya kujitambulisha mara baada ya kuteuliwa nafasi hiyo.

Amesema katika wizara yake anasimamia (Sera, Bunge na Uratibu) moja ya majukumu ni kuvisimamia vyama vya siasa hivyo atavitembelea vyama vyote 19.

Kwa upande wake, Msajili wa vyama vya siasa Jaji  Francis Mutungi pamoja na baadhi ya viongozi wa vyama vya siasa wamesema ziara hiyo itaongeza hamasa ya ushirikiano

Kiongozi Mkuu wa ACT-Wazalendo,Dorothy Semu amempongeza Waziri Lukuvi kwa kufanya ziara hiyo na kumuomba kuondoa hofu ya wananchi kuhusu kushiriki uchaguzi wa Serikali za Mitaa unaotarajia kufanyika Novemba mwaka huu.