Serikali kuendelea kuwezesha makundi ya kijamii kiuchumi

WAZIRI Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa amesema serikali itaendelea kuweka mazingira wezeshi kwa makundi ya kijamii kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi na kijamii.

Amesema serikali inafanya hivyo kwa kutambua kuwa, kundi la wajasiriamali ni muhimu na nguzo katika kukuza uchumi wa taifa kupitia shughuli zao.

Majaliwa amesema hayo wakati wa mkutano wake na makundi ya wajasiriamali Dar es Salaam.

“Nataka niwahakikishie serikali hii inanufaika nawe na ndio maana inaendelea kuwathamini na inapanga mipango mbalimbali juu yenu. Endeleeni kuimarisha biashara zenu, hatutawatupa,” amesema.

Amesema katika kuhakikisha kundi hilo linanufaika, serikali imetekeleza programu mbalimbali zenye lengo la kuwawezesha wajasiriamali nchini, ikiwemo utekelezaji wa programu za kuwezesha wananchi kupata mitaji, masoko na mafunzo ya ujasiriamali.

Nyingine ni Programu ya Taifa ya Uwezeshaji Wanawake Kiuchumi kusimamia uanzishwaji wa viwanda vidogo vidogo kupitia programu za uwezeshaji wajasiriamali, uendelezaji wa kongani za wajasiriamali pamoja na kutenga maeneo katika kila halmashauri kwa ajili ya shughuli za kilimo, viwanda, biashara na shughuli nyingine muhimu za kiuchumi.

Katika hatua nyingine, Majaliwa amesema serikali itaendelea kuweka msukumo wa kuhamasisha na kusimamia uanzishwaji na usajili wa vikundi vyenye mwelekeo wa ushirika na kampuni pamoja na kuwawezesha kupata mitaji na elimu ya matumizi ya mitaji hiyo ili waweze kuendesha shughuli zao kwa uhakika.

Majaliwa amesema serikali itaanzisha programu maalumu za kuwawezesha vijana waliomaliza taasisi za elimu ya juu na kati kuingia katika ajira na kujiajiri.

Naye Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalumu, Dk Dorothy Gwajima amesema kuwa anamshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa kusimamia maono yake ya kuhakikisha ananyanyua kundi la wajasiriamali ili yaende safari ndefu ya kumiliki uchumi wa Tanzania.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button