TANGA: WIZARA ya Kilimo imetoa vishikwambi 376 kwa maofisa kilimo waliopo Mkoa wa Tanga kwa ajili ya kukusanya taarifa za shughuli za kilimo kwenye maeneo yao.
Akikabidhi vishikwambi hivyo kwa wakuu wa Wilaya, Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Waziri Kindamba amesema kuwa vifaa hivyo vitumike kwa ajili ya kukusanya data za shughuli za kilimo.
“Kilimo ndio uti wa mgongo wa taifa hili hivyo vishikwambi hivi vikatumike katika kuleta mabadiliko katika sekta ya kilimo kwa kuhamishia matumizi ya data kiganjani badala ya mfumo wa kutumia makaratasi,” amesema RC Kindamba.
Amesema kuwa matarajio yake ni kuona maofisa ugani wanawafikia wananchi wengi na kusogeza huduma za ugani karibu na wananchi.
Naye Mkuu wa Wilaya ya Pangani, Zainab Abdallah amesema kuwa vifaa hivyo vinakwenda kuwa msaada mkubwa kwa wananchi kwani sasa maofisa ugani wataweza kupata taarifa za kwa wakati na kuzitoa kwa wananchi.
Naye Mkuu wa Wilaya ya Kilindi, Hashim Mgandilwa amesema kuwa taifa ili liendelee linahitaji uwekezaji kwenye kilimo hivyo uwepo wa vifaa hivyo utaboresha shughuli za kilimo.
“Sasa maofisa ugani wanakwenda kutumia vishikwambi hivyo kwaajili ya kupata taarifa za tafiti za kilimo na kuziwasilisha kwa wakulima.” Amesema DC Mgandilwa