DAR ES SALAAM: WIZARA ya Afya nchini imetoa tahadhari kwa wananchi kuacha kutumia dawa kiholela hususani tiba mbadala baada ya kuibuka kwa ugonjwa wa macho (red eyes) kwani tayari baadhi ya watu wameshaanza kupata madhara kwenye macho kutokana na matumizi hayo.
Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi wa Huduma za Tiba, Prof Paschal Ruggajo amesema tayari watu 12,332 waliofika katika vituo vya afya wamethibitika kupata ugonjwa huo huku ukienea zaidi ya mikoa 23 huku Mkoa wa Dar es Salaam ukiongoza kwa kuwa na watu 6,412, Pwani 4,041, Dodoma 363, Morogoro 307, Mtwara 193, Shinyanga 193,T anga 190, Lindi 101.
Mikoa Mingine ni Katavi 94, Njombe 81, Ruvuma 77,Arusha 42, Mwanza 40, Mbeya 37, Songwe 33, Rukwa 31, Kilimanjaro 31, Geita 18, Singida 17, Kigoma 13 ,Simiyu tusa,Mara tano na Tabora nne.
Amesema wizara ikikemea vikali tabia ya wananchi kutumia mitandao ya kijamii kama taarifa rasmi zinazohusu afya zao na tiba.
Ruggajo amesema wamepokea taarifa kutoka vituo vya afya kuna ongezeko la wagonjwa wanaofika wakiwa na vidonda kwenye kioo cha mbele cha jicho walizopata baada ya kutumia tiba zisizo rasmi au ambazo hazijaandikwa na daktari rasmi kutubu macho.
“Baadhi ya vitu vinavyotumika ni pamoja na dawa zenye vichoche vya steroids wanakwenda kununua wenyewe kwenye maduka ya dawa,wanatumia tangawizi,majani ya chai yaliyokolea,mafuta tete yaliyokuwa yanatumika wakati wa Covid-19,maji ya chumvi na maziwa ya mama.
Ameongeza”Wizara katika tamko lake la awali ilitamka wazi kuwa wananchi wasitumie dawa zisizo rasmi wala tiba mbadala wanapopata red eyes na badala yake waende vituo vya kutolea huduma za afya.