Tanzania yaongeza udhibiti sekta ya madini

DAR ES SALAAM: Tanzania inaongeza juhudi za kuimarisha ushawishi wa serikali katika sekta ya madini, huku ikilenga kuongeza faida za ndani zinazotokana na rasilimali hizo, wakati nchi nyingi za Afrika zikisukuma mbele ajenda ya kuwa na udhibiti mkubwa wa rasilimali muhimu zinazohitajika duniani, hasa katika kipindi hiki cha mpito wa nishati safi.
Tanzania ambayo ni miongoni mwa wazalishaji wakubwa wa madini ya dhahabu Afrika, na pia inaibukia kama msambazaji wa madini muhimu kama grafiti, nikeli na madini adimu (rare earth), imekuwa ikitekeleza sera zinazolenga kuongeza ushiriki wa wazawa, kupanua uchakataji wa madini ndani ya nchi na kuimarisha usimamizi wa serikali katika sekta hiyo.
Mwelekeo huu ni sehemu ya mkondo mpana barani Afrika unaojulikana kama “utaifishaji wa rasilimali” (resource nationalism), ambapo serikali zinataka kupata faida kubwa zaidi kiuchumi, umiliki mpana na udhibiti wa rasilimali ambazo kwa muda mrefu zilikuwa zikimilikiwa zaidi na wawekezaji wa kigeni.
Waziri wa Madini, Anthony Mavunde, amesema lengo la Tanzania ni kuhakikisha sekta ya madini inachangia moja kwa moja katika viwanda, ajira na mabadiliko ya uchumi wa taifa.
Alisema, “Tunataka rasilimali za Tanzania ziongeze thamani ndani ya nchi kupitia uchakataji, uhamishaji wa teknolojia na ushiriki wa wazawa.”
Sera hiyo pia inaendana na wito wa Southern African Development Community (SADC), unaohamasisha nchi za Afrika kushirikiana katika maendeleo ya madini na kujadiliana kwa nguvu ya pamoja kadri ushindani wa kimataifa wa kupata madini muhimu unavyoongezeka.
Barani Afrika, serikali nyingi sasa zinajaribu kuepuka kuwa wasafirishaji wa malighafi pekee, huku nchi zilizoendelea zikinufaika zaidi kupitia viwanda vya thamani ya juu kama vile magari ya umeme, hifadhi ya nishati na teknolojia za nishati jadidifu.
Nchini Tanzania, mwelekeo wa utaifishaji wa rasilimali uliongezeka baada ya mageuzi makubwa ya sekta ya madini yaliyofanyika katika miaka ya hivi karibuni. Mageuzi hayo yalihusisha kuongeza hisa za serikali katika miradi ya madini, kuimarisha udhibiti wa usafirishaji wa madini nje ya nchi, na kupanua masharti ya ushiriki wa wazawa (local content).
Serikali pia imekuwa ikihamasisha uchakataji wa madini ndani ya nchi, ikiwemo uchenjuaji wa dhahabu na mipango ya kuongeza miundombinu ya kuongeza thamani kwa madini yanayotumika kwenye betri.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mahmoud Thabit Kombo, amesema Afrika inapaswa kuhakikisha rasilimali zake zinatumika kwa manufaa ya maendeleo ya muda mrefu badala ya kunufaisha viwanda vya nje pekee.
Amesema kuna uelewa unaoongezeka kuwa Afrika lazima ilinde maslahi yake ya kiuchumi huku ikiendelea kuwa wazi kwa uwekezaji wenye tija.
Wachambuzi wanasema Tanzania inajaribu kusawazisha kati ya kuvutia uwekezaji wa kigeni na kukidhi shinikizo la ndani la kutaka udhibiti mkubwa wa rasilimali za taifa.
Kwa mujibu wa mchambuzi mmoja wa sera za madini jijini Dar es Salaam, ushindani wa kimataifa wa kupata madini muhimu umeongeza nguvu ya majadiliano kwa nchi za Afrika zenye rasilimali nyingi. Serikali sasa zinaona madini si bidhaa za kuuza nje tu, bali pia kama rasilimali za kimkakati na kisiasa.
Umuhimu unaoongezeka wa madini kama grafiti, nikeli na madini adimu umeifanya Tanzania kuwa na nafasi muhimu kimkakati, huku mataifa makubwa kama China, Marekani na Umoja wa Ulaya yakishindana kupata uhakika wa upatikanaji wa madini hayo.
Hata hivyo, wawekezaji wanaendelea kuonya kuwa mabadiliko yasiyotabirika ya sera, migogoro ya kodi na kuingilia kwa serikali vinaweza kuathiri maamuzi ya uwekezaji wa muda mrefu.
Katika miaka ya karibuni, Tanzania imejaribu kuboresha mahusiano na wawekezaji wa kimataifa baada ya migogoro ya awali kuhusu mikataba ya madini na mgawanyo wa mapato.
Utawala wa Rais Samia Suluhu Hassan umejitahidi kujenga taswira rafiki kwa wawekezaji, huku ukiendelea kusimamia sera kuu za kuhakikisha taifa linapata faida kubwa zaidi kutoka kwenye rasilimali zake.
Wataalamu wa kikanda wanaona kuwa utaifishaji wa rasilimali utaendelea kuwa sehemu muhimu ya sera za uchumi barani Afrika, huku nchi zikilenga kutumia utajiri wa madini kujenga viwanda na kuongeza nguvu ya majadiliano katika soko la kimataifa.



