Tanzania yasisitiza urejeaji wa hiari suluhisho kwa wakimbizi

USWISI: Tanzania imesisitiza kuwa urejeaji wa hiari ndilo suluhisho sahihi na la kudumu kwa wakimbizi, ili kufanikisha lengo la kupunguza idadi ya wakimbizi kwa 50% ifikapo 2035.

Juni 16, 2026, Tanzania ilishiriki Mkutano wa 96 wa UNHCR Standing Committee unaoendelea mjini Geneva, Uswisi. Katika mchango wake kuhusu Taarifa ya Hifadhi ya Ukimbizi Duniani iliyowasilishwa na UNHCR, Tanzania imeipongeza UNHCR kwa kazi nzuri inayotekelezwa duniani kote, ikiwemo ndani ya Tanzania, licha ya changamoto za kifedha zinazoendelea.

Tanzania imeeleza hali halisi inayoikabili mifumo ya hifadhi ya wakimbizi kwa sasa, ikiwemo mwenendo wa baadhi ya wakimbizi kujichagulia suluhisho za kudumu wanazozitaka bila kuzingatia uhalisia wa mazingira. Hata pale sababu za awali za kukimbia zikiwa hazipo tena, baadhi yao wanagoma kurejea kwa hiari kwa sababu tu “hawataki,” huku wakiendelea kuvuka mipaka kurejea nchi zao za asili kwa shughuli za kijamii au kusimamia uwekezaji, na baadaye kurejea katika nchi inayowahifadhi.

Tabia hii inadhoofisha juhudi za kupata suluhisho za kudumu.Kuhusu suluhisho za kudumu, Tanzania ikiwakilishwa na Mkurugenzi wa Wakimbizi Tanzania Bwana Sudi Mwakibasi na Naibu Mwakilishi wa Kudumu Balozi Dk Hoyce Temu, imesisitiza kuwa urejeaji wa hiari ndilo suluhisho linalotekelezeka zaidi katika kufanikisha lengo la kupunguza idadi ya wakimbizi kwa 50% ifikapo 2035.

Njia nyingine kama utangamanishaji katika nchi ya ukimbizi au uhamisho kwenda nchi ya tatu zinategemea sana mazingira ya kimaamuzi ya nchi husika, huku sera za uhamiaji duniani zikizidi kuwa za kubana.

Aidha, Tanzania iliwasilisha taarifa kuhusu makubaliano ya kuanza urejeshaji wa wakimbizi wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) kwa hiari katika maeneo salama ndani ya nchi hiyo. Hata hivyo, changamoto kubwa iliyobainishwa ni upatikanaji wa fedha kwa ajili ya zoezi la uhakiki ili kubaini idadi sahihi ya wakimbizi na maeneo wanayopendelea kurejea. Tanzania imeiomba UNHCR na jumuiya ya kimataifa kufadhili zoezi hili kwa dharura ili kuendeleza mwelekeo wa kufanikisha lengo la 50% ifikapo 2035.a

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button