TP Mazembe ya mwisho kufuzu Ligi ya Mabingwa

TIMU ya wanawake ya TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) imekuwa timu ya mwisho kufuzu kwa Michuano ya Ligi ya Mabingwa wa Afrika.
TP Mazembe sasa itashiriki michuano hiyo ya Afrika, ambayo itafanyika Morocco kuanzia Oktoba 30 hadi Novemba 13, 2022.
Timu hiyo iliifunga timu ya Cameroon ya AS AWA FC kwa mabao 2-1 katika fainali ya Mataifa ya Afrika ya Kati (UNIFFAC), shukrani kwa mabao kutoka kwa Justine Onderumbu Bousu (31′) na Merveille Kanjinga (82′), bao pekee la Cameroon lilifungwa na mchezaji wa kimataifa, Farida Machia katika dakika ya 52.
Kufuzu kwa TP Mazembe kuna maana kuwa sasa klabu zote nane zitakazoshiriki fainali nchini Morocco zimekamilika.
Timu hiyo ya Congo imepangwa pamoja na mabingwa watetezi ya wanawake ya Mamelodi Sundowns ya Afrika Kusini, Bayelsa Queens ya Nigeria na Wadi Degla ya Misri katika Kundi B.
Kundi A: Litakuwa na wenyeji Morocco, ambao ni washindi watatu wa michuano ya mwaka jana, ambao watakutana na Simba Queens ya Tanzania, Green Buffaloes ya Zambia na Determine Girls wa Liberia.
Fainali za mwaka huu za Michuano ya Caf kwa wanawake za Ligi ya Mabingwa wa Afrika zitafanyika nchini Morocco.