TRA yapania kuboresha huduma kwa wafanyabiashara

KATAVI; Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) mkoani Katavi imeadhimisha Wiki ya Huduma kwa Wateja kwa lengo la kusikiliza maoni, changamoto na mapendekezo kutoka kwa wananchi na wadau wa biashara, ili kuboresha utoaji wa huduma zake.
Akizungumza wakati wa uzinduzi huo uliofanyika ofisi za TRA mkoani humo, Kaimu Meneja wa TRA Mkoa wa Katavi, Clemence Kamara amesema wiki hiyo ni sehemu ya kuimarisha uhusiano kati ya mamlaka hiyo na wateja wake, sambamba na kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa kulipa kodi kwa hiari.
“Tutaboresha huduma kwa kurahisisha mifumo ya kodi, sheria za kodi ziweze kutekelezeka kwa urahisi ndio maana huwa tunapokea maoni yenu,” amesema.

Amebainisha kuwa katika kipindi chote cha maadhimisho hayo, TRA Katavi itatoa elimu kuhusu matumizi ya mifumo ya kidijitali pamoja na huduma mbalimbali zinazopatikana bila malipo, ikiwemo ushauri wa kodi na usajili wa walipa kodi wapya.
Wakizungumza kwa niaba ya wafanyabiashara mkoani humo, viongozi wa wafanyabiashara Hasanari Dallah na Aman Mahela wamesema hatua hiyo ni chachu ya kuboresha uhusiano kati ya mamlaka na wateja, huku wakipongeza jitihada za maafisa wa mamlaka hiyo kwa kutoa huduma kwa ukaribu na heshima.
“Kikubwa zaidi ni kutanguliza utu, hakuna aliye mkamilifu, sisi wafanyabiashara hatukusomea biashara ila tunategemea elimu ya biashara tuipate kutoka kwenu, hivyo msichoke kutupatia elimu kwa kuwa kila mwaka wafanyabishara wapya wanaongezeka,” amesema Mahela.

“Huduma zimeboreshwa sana, tunapata maelezo kwa uwazi na tunafundishwa namna ya kutumia mifumo ya malipo ya kodi, jambo linalorahisisha biashara zetu,” amesema Saida Hamisi mmoja wa wafanyabiashara wa mjini Mpanda.



