Tume kufuatilia madawati ya Jinsia vyuoni, shuleni yaundwa

WIZARA ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia , Wanawake na Mkundi Maalum inatarajia kuunda tume ambayo itazifuatilia  taasisi za elimu ya juu na elimu ya kati kuona endapo zimefungua madawati ya Jinsia ukiwa ni  utekelezaji wa agizo la  serikali.

Naibu waziri wa wizara hiyo ,Mwanaidi Ali Khamis alisema hayo  Februari 10, 2023   mjini Morogoro wakati akifungua mafunzo ya namna bora ya uanzishaji na uendelezaji wa madawati ya jinsia katika vyuo  kwa wakuu wa vyuo na waratibu wa madawati hayo kwa vyuo kutoka mikoa ya Tanga , Pwani na Morogoro.

Advertisement

Tume hiyo itafuatilia utekelezaji wa agizo la  Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa alilolitoa  Novemba 25, 2021 Jijini Dar es Salaam alipozindua  kampeni ya siku 16 ya kupinga ukatili wa kijinsia na kuelekeza vyuo vyote nchini kuanzisha madawati ya kijinsia kwa ajili ya kutokomeza aina zote za ukatili maeneo ya vyuo .

Naibu Waziri alisema serikali kwa kushirikiana na wadau inemuwa ikitekeleza mpango kazi wa Taifa wa kutkomeza ukatili dhidi ya wanawake na watoto ( MTAKUWWA) wa mwaka 2017/2018 – 2021/2022 ambapo muda wake umeisha Juni , 2022.

Mbali na hayo alisema mpango wa Mtakuwwa awamu ya pili wa mwaka 2023/2024- 2027/ 2028 unatarajia kuanza  kutekelezwa muda sio mrefu na serikali imechukua jitihada mbalimbali za kukabiliana  na vitendio vya ukatili na unyanyasaji wa kijinsia.

Naibu Waziri alisema  miongoni mwa jitihada hizo ni pamoja na kuanzishwa madawati ya kijinsia katika taasisi ya elimu ya juu na elimu ya kati hapa nchini

“ Dawati hili litakuwa ni nyenzo muhimu ya kuweka ulinzi na mfumo wa kushughulikia matukio ya ukatili na unyanyasaji wa kijinsia katika vyuo ikiwemo rushwa ya ngono kwani vitendo hivi havikubaliki kwa kuwa madhara yake ni makubwa “ alisema Mwanaidi

Naibu Waziri  aliyataka taasisi za elimu ya juu na elimu ya kati ambayo tayari yameazishwa madawati hayo kuhakikisha yanafuatilia kwa ukaribu vishiria na vitendo vya ukatili na kuchukua hatua stahiki.

Pia aliagiza  madawati ya jinsia yanayofunguliwa katika   vyuo yatumike kikamilifu kutoa elimu itakayowasaidia wanafunzi  kujiamini  katika maisha yao bila kupata bughudha  na hofu ili waweze patikana viongozi bora watakao kuja kuiongoza nchi yetu.

Naye  Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Waislamu cha Morogoro  (MUM) , Profesa Mussa Assad , alisema wanafunzi wengi wa mwaka wa  kwanza wanapoingia  vyuoni  huwa hawajitambu vizuri  “ulimbukeni” hususani  wakike na wanaingia kwenye  majaribu mengi kutoka kwa vijana wa kiume vyuoni na wengine wa  mitaani .

 Mimi kwa uzoefu wangu wa miaka miwili hapa Morogoro ni muhimu sana kuanzisha madawati ya jinsia kwenye vyuo ili kuwapa uelewa watoto wetu  kuelezea maadili ya walimu na katika hilo  ndani ya MUM  halina nafasi kwa mwalimu anayehisiwa na taarifa za uhakika zinapopatikana kushiriki vitendo viovu anaondolewa mara moja “ alisema Profesa Assad

Naye Mkuu wa Chuo cha Polisi Kidatu, Kamisha Msaidizi wa Polisi , Zarau Mpangule   alisema mmomonyoko wa maadili  katika jamii ni  chanzo kikubwa cha kushamiri kwa vitendo vya ukatili wa kijinsia na vinachangiwa na kuunga utamaduni wa kimagharibi .

Mpangule  alisema ili kupunguza ama kutomomeza vitendo hivyo ni vyema elimu ya kupinga ukatili wa kijinsia katika jamii iwe ni endelevu na katika kiwango kikubwa.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Jinsia , Rennie Gondwe alisema mafunzo hayo  yaliwashirikisha washiriki 115 wakiwemo wakuu wa vyuo  na waratibu wa madawati ya jinsia wa  mikoa Tanga , Pwani na Morogoro ambayo ni mwendelezo kwa nchi mzima na yalianza  katika  mkoa wa  Dar es Salaam.

Add a comment

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *