“NIMEZALIWA katika Kijiji hiki cha Imbaseni miaka 74 iliyopita ,changamoto kubwa na ya muda wote ni huduma za afya na ubovu wa hili barabara lakini katika umri wangu huu tayari nimeshaanza kuona matumaini kwa upande wa matibabu,”anasimulia mzee Zakari Mbise mwenye umri wa miaka 74.
Mbise ambaye pia ni mwanajeshi mstaafu anasema baada ya wananchi kukumbwa na kero kubwa ya huduma za matibabu kwa muda mrefu mwaka 2016 waliitisha kikao cha kijiji chenye lengo la kuanza mazungumzo ya kuchanga kwaajili ya kujenga zahanati ya kijiji.
Umbali kutoka kijiji cha Imbaseni hadi kufikia kituo cha afya cha Usa River ni zaidi ya kilometa 12 huku kijiji hicho kikikabiwa na ubovu ya barabara na isiyopitika hasa wakati wa masimu wa mvua.
Mbise anasema iwapo mgonjwa au mama anayetaka kujifungua akitoea hasa majira ya usiku zoezi la kumfikisha kituo cha afya linaweza kukwama na wakati mwingine mama mjamzito kujifungua barabarani au kupoteza maisha kabisa.
Kwa mujibu wa Mbise Mkutano huo ulifanikiwa baada ya wananchi kukubaliana kwa sauti moja kutoa michango.
Kijiji cha Imbaseni Kilichopo katika kata ya Imbaseni,Wilaya ya Meru, mkoani Arusha kina jumla ya wanakijiji 29,770 ambao walianza kujenga jengo la zahanati mwaka 2016.
“Waliweza kutoa michango mbalimbali kwa kuanza na mawe ,walijitolea fedha ,mwenyekiti alitembea kwa wadau mbalimbali kuomba fedha kwaajili ya ujenzi na baadae viongozi wakaona ni vizuri kwenda kwa serikali kwaajili ya kupata eneno ambalo lilikuwepo mda mrefu na ikaidhinishwa kituo kijengwe,”anaeleza Mbise.
Kiasi cha Sh milioni 23.6 ambacho kilichangwa kutoka kwa wananchi na wadau kiliweza kufikisha ujenzi kwa hatua ya lenta ambapo baada ya hapo ujenzi ulisimama.
SERIKALI YAINGILIA KATI
Ofisa Mtendaji wa Kata ya Imbaseni,John Panga anasema baada ya kusuasua kwa ujenzi mwaka 2021 waliweza kupata fedha kutoka serikali na kuendelea na ujenzi hadi hatua ya kumalizia.
“Tulipofika hatua ya lenta tulipata hela ya serikali kupitia mfuko wa pamoja wa vituo vya afya vya msingi (Health Busket Fund) kiasi cha Sh milioni 50 kwa mara ya kwanza na mara ya pili Sh milioni 15 jumla Sh milioni 65.
Panga aliishukuru serikali kwa kutoa fedha hizo ambapo jengo sasa limefika katika hatua nzuri na kusema kuwa uwepo wa zahanati hiyo utasaidia wakazi wa Imbaseni na majirani.
“Kwa hapa karibu vituo vya afya viko mbali hivyo ni msaada mkubwa hasa kwa wanawake wanapokuwa katika hatua za kujifungua zingine ziko kilometa zaidi ya 10.
Anasema ili zahanati hiyo ikamilike na kunza ktumika inahitaji kiasi cha Sh milioni 20,vifaa tiba na watoa huduma za afya.
MAFANIKIO MAKUBWA AFYA MERU
Katika kipindi cha miaka miwili iliyopita Wilaya ya Meru imepokea jumla ya Sh bilioni 1 .5 kwaajili ya kuboresha miradi ya maendeleo yanayohusiana na huduma za afya .
Kaimu Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Wilaya hiyo, Dk Wyliffe Sango anasema Katika hospitali ya Wilaya ya Meru (Patandi) serikali imejenga jengo la huduma za dharura ambapo wanahudumiwa wagonjwa saba kwa wakati mmoja wakiwa katika hali ya mahututi.
Dk Sango anaeleza kuwa jengo hilo liligharimu Sh milioni 300 kukamilika ambapo pia Sh milioni 875 zilitolewa kwaajili ya vifaa vinavyotumika katika jengo hilo.
“Kuna mashine na mitambo ambapo hapo awali havikuwepo na hospitali haikuwa na uwezo wa kutoa huduma kwa kiwango hicho na limeanza kutumika mwaka 2023 sasa tuna uhakika mgonjwa akija hata akiwa katika hali mahututi tunaweza kumuhudumia vizuri na tukiendelea kufuatilia maendeleo yake tunatumia mashine maalum za ufuatiliaji inajua kila hatua ya mgonjwa na kama kuna changamoto mashine zinatuongoza.
Anasema jengo hilo muhimu lina vyumba vya watoto na watu wazima wanawake na wanaume na kuna mitambo ya mawasiliano kwa kila chumba kwa mtu aliyeko katika kituo kikuu anapata taarifa za wagonjwa wote.
Miradi mingine iliyojengwa ni Kuna Zahanati ya Maji ya Chai ambapo kiasi cha Sh milioni 90 zilitumika na nyumba moja za watumishi ambapo wanaweza kukaa watatu.
“Kuna kituo cha afya cha Mareu ambacho kilipata milioni Sh milioni 500 hapo awali kulikuwa na jengo moja dogo la vyumba vitatu na zamani ilikuwa zahanati ikageuzwa kuwa kituo cha afya kwasababu ya umbali.
Anaongenza “Lakini pia majengo yalikuwa hayatoshelezi sasa Sh milioni 500 imesaidia kujenga jengo la wagonjwa wa nje ,maabara,jengo la mama na mtoto,chumba cha upasuaji na wodi hivyo huduma zimeboreka na zimekuwa na kisasa.
Anabainisha kuwa hapo awali katika hospitali ya Wilaya kwa mwezi kilikuwa unaweza kuona wagonjwa 200 hadi 300 lakini sasa wanafika 2000 hadi 3000 na kwa magonjwa ya dharura wagonjwa wengi awali waliku wanapelekwa hospitali ya rufaa ya mkoa na Hospitali ya Rufaa ya Kidini Seliani.
“Sasa kwa mwezi wagonjwa wa nje wameongezeka kutoka 3000 mpaka 5000 kwa mwezi inaonesha kuboresha huduma inaongeza idadi ya watu wanaofata huduma kwasababu zisingekuwa bora wasingekuja wangeenda hospitali ya mkoa.
Dk Sango anasema kwa zahanati zingine walipata Sh milioni 250 kwa ajili ya kukamilisha ujenzi ambazo ni kuna Medusosia ,Milandini,Maji ya chai, Migungani na Shistoni.
“Hizi zilikuwa zimejengwa kufikia hatua ya lenta wananchi walianza kwa nguvu zao lakini serikali ilivyoongeza kila zahanati ilipata Sh milioni 50 na zahanati karibu zote zimeanza huduma.
Anasema walipata Sh milioni 43 kwaajili ya ujenzi wa idara ya mionzi katika kituo cha afya Mbuguni na tumepewa fedha zingine milioni 160 kwaajili ya kupanua huduma ya mama na mtoto.
“Tumepokea Sh milioni 900 tofauti na Sh bilioni 1.5 hizo zimeletwa kuboresha huduma katika hospitali ya wilaya na kujenga jengo la kisasa la wagonjwa wa nje,kukarabati majengo ya zamani na kuweka mitambo ya kuchomea taka hatarishi.
MIKAKATI ZAIDI
Dk Sango anasema mikakati zaidi ni kuendeleza watumishi wa afya kwa kuwapatia elimu hasa kwa magonjwa yanayoendelea sasa na kuwaendeleza kutumia vifaa na mitambo wanayopata sasa na kuendelea kutanua huduma mbalimbali ili mgonjwa asihangaike kwenda mbali.
“Idadi ya madaktari bado hajitoshelezi lakini ndani ya miaka miwili tumepata madaktari 40 ukiacha wahudumu wengine imeongeza nguvu kazi japo hawatoshi kabisa.
WAMSHUKURU RAIS SAMIA
Mkazi wa kijiji cha Imbaseni ,Grace John anamshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa kumalizia zahanati yao ambayo ilikwama kwa muda mrefu.
“Tunashukuru kupata zahanati na tunafurahi maana ilikuwa tunateseka hasa akinamama wajawazito wanajifungulia njia kutokana na barabara kuwa na mawe mengi tumeteseka vyakutosha, tunaomba atuharakishie tuanze mapema hata mwaka huu usiishe ianze kufanya kazi alete madakatri,vifaa tiba ili tupate huduma kwa wepesi.
Anasema zahanati ikiwa tayari watafanya sherehe kwasababu wamechoka kuteseka na watu wengine wanapoteza maisha barabarani kwasababu ya umbali wa huduma.
“Tunaomba mama yetu mpendwa Rais Samia atusaidia zaidi tuweze kumaliza zahanati yetu ianze kufanya kazi tupate huduma.
Mbise anasema wanaishukuru serikali kwani walitoa fedha na kuchangia ujenzi wa jengo hilo na kufikia hatua za kukamilika .
“Jengo hili tunamatumaini kuwa itatusaidia kuweza kupata matibabu kwa wagonjwa na wajawazito hapa tunategemea kupata msaada hivi karibuni,namuomba Rais atusaidie tena kumalizia jengo hili ili tuweze kupata huduma na kupata viafaa tiba na kupata madaktari,”alieleza Mbise.