Vifaa vya kieletroniki mkombozi kwa walimu

DAR ES SALAAM: TAASISI ya Shanghai EDUTECH ya nchini China imetoa vifaa vya kielektroniki kwa ajili ya kuboresha eneo la ufundishaji na ujifunzaji nchini.

Vifaa hivyo vimekabidhiwa leo Desemba 6, 2023 jijini Dar es Salaam kwa Mkurugnezi wa elimu ya msingi kutoka Ofisi ya Rais Tawala za Miko ana Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Susan Nusu ambaye pia alivikabidhi kwa Shirika la Elimu Kibaha, Taasisi ya Elimu Tanzania (TET) na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar.

Akizungumza mara baada ya kupokea vifaa hivyo, Susan amesema vitasaidia katika ufundishaji wa madarasa ya kisasa ‘smart class room’ na vitasaidia kuboresha eneo la ufundishaji na ujifunzaji nchini.

Advertisement

Amesema, vifaa hivyo vitafungwa katika madarasa hayo na kuwezesha walimu zaidi ya 10,000 kupata mafunzo kiurahisi wakiwa katika mikoa mbalimbali na kuongeza ufanisi katika elimu.

“Ni imani yangu vifaa hivi vitatumika ipasavyo katika kuleta matokeo chanya kwenye elimu,naomba mhakikishe kuwa walimu wengi zaidi wanafikiwa kupitia mafunzo kwenye madarasa hayo,” amesema Susan.

Nae, Mkurugenzi Mkuu wa TET, Dk Aneth Komba amesema kuwa ni jambo la muhimu kwa vifaa vya madarasa hayo kukabidhiwa kwa wahusika ambavyo vimekuja sambamba na maboresho ya mtaala ambayo msisitizo wake ni kwenye matumizi ya TEHAMA katika ufundishaji na ujifunzaji.

Amesema, walimu wengi sasa nchini watafikiwa kwa haraka kutokana na mafunzo hayo ambayo yatakwenda kuongeza chachu katika elimu.

Naye, mwakilishi wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar, Sauda Abdullah Haji ameshukuru kwa msaada huo ambao amesema kwamba utawezesha walimu nchini kupata mafunzo yanayoendana na mabadiliko kutokana na matumizi ya TEHAMA kuwa ya kiwango kikubwa.

1 comments

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *