DR CONGO : UJUMBE wa taasisi mbili za kanisa nchini Jamhuri wa Kidemokrasi ya Congo umekutana na waasi wa M23 mashariki mwa taifa hilo katika juhudi za kusaka amani na mazungumzo baada ya wiki kadhaa za mapigano.
Ujumbe huo wa pamoja kutoka Baraza la Maaskofu wa Kanisa Katoliki nchini Congo na ule wa Kanisa la Kristo la Congo uliwasili Goma siku ya Jumatano na kukutana na kiongozi wa kisiasa wa kundi la M23, Corneille Nangaa.
Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu la Congo, Askofu Donatien Nshole, amesema mkutano na M23 ulikuwa na nafasi ya kutafuta njia za kumaliza vita haraka iwezekanavyo.
Amesema taasisi hizo mbili kubwa za kidini zinaamini mzozo unaoendelea nchini humo hautamalizwa kwa njia za kijeshi. SOMA: Congo yaipelekea Rwanda mahakamani
Mkutano huo umefanyika wakati inaarifiwa waasi hao wanaoungwa mkono na Rwanda wanaendelea na mapigano wakisonga mbele kuelekea mji mkuu wa jimbo la Kivu Kusini wa Bukavu.