Visima 150 kuchimbwa kilimo cha imwagiliaji Geita

GEITA: SERIKALI kupitia Tume ya Taifa ya Umwagiliaji (NIRC) imeweka mpango wa muda mrefu wa kuchimba visima 150 katika halmashauri za mkoa wa Geita ili kukuza sekta ya kilimo kupitia wakulima wadogo.
Mradi wa visima ni sehemu ya mradi kilimo cha umwagiliaji unaohusisha usanifu na ujenzi wa mabwawa, visima na skimu za umwagiliaji wenye thamani ya takribani Sh bilioni 37.34 unaotekelezwa mkoani Geita.
Awamu ya kwanza ya mradi inahusisha uchimbaji wa visima 36 katika vijiji 32 kwenye eneo la hekari 1,440 lenye wakulima zaidi ya 747 na utekelezaji utaanza na visima 30 vilivyofanyiwa tathimini.

Mhandisi wa Umwagiliaji mkoani Geita, Boniface Mkita ametoa taarifa hiyo katika uzinduzi wa mradi uliofanyika Kijiji cha Mwilima kata ya Kanyala mjini Geita ambapo utekelezaji umeanza na visima 30 vilivyofanyiwa tathimini.
“Lengo la visima hivi ni kupambana na mabadiliko ya tabia ya nchi ikiwemo mvua zisizotabirika ili kuongeza uzalishaji wa mazao kwa wakulima wadogo kupitia kilimo cha umwagiliaji”, amesema Mhandisi Mkita.
Mhandisi Mkita amesema shughuli ya uchimbaji wa visima inatekelezwa na NIRC kwa kushirikiana na halmashauri husika ambapo ndani ya wiki mbili zoezi la uchimbaji visima hivo linatarajiwa kukamilika.

Amefafanua kuwa katika mradi huo NIRC itahusika kuchimba kisima chenye urefu usiozidi mita 250, kuweka mabomba yenye kipenyo cha inchi 6 hadi 8 na ufungaji wa mfumo mkuu wa upelekaji wa maji shambaji.
Ameongeza kuwa, pia NIRC itaweka tenki la maji lenye uwezo wa kuhifadhi lita 10,000 sambamba na uwekaji wa nishati kwa ajili ya uendeshaji ya uendeshaji wa pampu za maji ya umwagiliaji mashambani.
“Wakulima watapata huduma hii kwa ruzuku ya asilimia 100 inayotolewa na serikali, wakulima watakaonufaika na huduma hii watakuwa katika vikundi vinavyotambulika na halmashauri”, amesema.
Amesema serikali tayari imetoa mtambo mitano ya kuchimba visima kwenye awamu ya kwanza kwenye halmashauri sita mkoani Geita, ambapo kila halamshauri itaanza kwa kupata visima vitano.
Katibu Tawala wa wilaya ya Geita, Lucy Beda amesema mradi huo utanufaisha wananchi wengi ambo ni wakulima waliokuwa wanaendesha shughuli zao kwa kutegemea mvua za masika na mvua za vuli.
Mkuu wa mkoa wa Geita, Martine Shigela ameagiza Idara ya Kilimo na Mifugo kusimamia mradi huo kwa ufanisi kwa kufanya vipimo udongo vya maeneo ili wakulima wapate maji na kutumia mbolea sahihi.
Mwenyekiti wa Kijiji cha Mwilima, Nyanda Samson amesema mradi huo ni mkombozi kwa wakulima wa wa mazao ya nafaka hususani mpunga na mahindi ambapo watalima bila kutegemea mvua.



