Wakulima sasa kupanda, kufukia kwa kutumia mashine

UTAFITI wa kutengeneza teknolojia ya kuwawezesha wakulima kupanda kwa nafasi sahihi na kwa muda mfupi zao la pamba umekamilika.

Mtafiti kutoka Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI), Kituo cha Ukiliguru jijini Mwanza, Dawson Malela amesema hayo alipokuwa akizungumza na HabariLEO.

Malela amesema watafiti kutoka TARI Ukiliguru walitafiti teknolojia ya mashine ambayo ina uwezo wa kuchimba mashimo yenyewe na kwa nafasi ya sentimita 60, lakini pia inaweka mbegu kwa hatua za sentimita 30 kutoka mmea hadi mmea.

Advertisement

“Mbali na kuchimba mashimo, kuweka mbegu pia teknolojia hiyo inafukia mbegu hizo.

“Kwa kutumia teknolojia hii sasa mkulima ana uwezo wa kuhakikisha mbegu zimepandwa kikamilifu bila kuwa na vibarua wengi,” amesema.

Ameongeza kuwa teknolojia hiyo inatumia saa moja kwa eneo la ekari moja huku ikiongozwa na mtu mmoja tu.

“Tofauti na wakulima walivyokuwa wakipanda eneo la ekari moja kwa kutumia jembe la mkono. Hapo  walitakiwa wakulima kati ya nane mpaka tisa tena wakitumia muda wa saa nane mpaka tisa.

“Sasa hii inaenda kuwa mkombozi kwa upande wa muda kwa sababu inatumia muda wa saa moja wakati kupanda kwa jembe la mkono saa nane mpaka tisa,” amesema.

Kwa maelezo mengine amesema itaondoa gharama za vibarua kwa sababu wastani kwa kibarua mmoja kwa siku ni sh 4000.

“Kwa hiyo ukiwa nao nane unazungumzia sh 32,000 na kuendelea. Wakati hii ‘planter’ inatumia lita moja ya petrol eneo la ekari moja.

“Thamani ya lita moja ni wastani wa sh 3,200 , operator ni mmoja anawezalipwa sh 5000 sasa sh. 5,000 ukijumlisha sh 3,000 inakuwa ni sh 8,000 ambayo ni gharama nafuu sana.

“Pia inakomboa muda kwa hiyo wakati wa kupanda vibarua wakisumbua ukiwa na mashine hiyo utapanda kwa wakati na ukahakikisha msimu imeuwahi,” amesema.

Amesema wazo la teknolojia hiyo ya kupanda pamba lilianza Agosti mwaka jana.

Amesema mwanzoni wakulima wa zao la pamba walipanda zao hilo kwa nafasi ya sentimita 90 kutoka mstari hadi mstari, na sentimita 40 kutoka mmea hadi mmea.

Lakini sasa utafiti umeibua teknolojia hiyo mpya ambayo upandaji ni sentimita 60 toka mstari hadi mstari na sentimita 30 kutoka mmea hadi mmea.

Amesema teknolojia hiyo mpya umewezesha mbegu kupandwa kwa nafasi ya sentimita 60 kwa 30 inayomfanya mkulima kuwa na mimea 44,444 mara mbili ya nafasi ya kwanza.

3 comments

Comments are closed.