Wanaopiga kura Zanzibar leo watajwa

ZANZIBAR; BAADHI ya wananchi wa Zanzibar leo wanapiga kura ikiwa ni sehemu ya uchaguzi mkuu wa mwaka huu.

Katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu Zanzibar kuna vituo 2,547 vya kupigia kura katika majimbo 50.

Kampeni za uchaguzi Zanzibar zilianza Agosti 28 na zilihitimishwa jana.

Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Jaji wa Rufani mstaafu, Jacobs Mwambegele alisema Zanzibar kuna kura ya mapema kwa sababu sheria inaruhusu lakini Tanzania Bara haina kura ya aina hiyo kwa sababu hakuna sheria inayoruhusu kufanya hivyo.

Kifungu cha 82 cha Sheria ya Uchaguzi Namba 4 ya mwaka 2018 kimetaja watu na taasisi zinazohusika na upigaji wa kura ya mapema wakiwemo wajumbe wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC).

Sheria imeeleza Tume itaweka utaratibu utakaoruhusu upigaji wa kura mapema ambao utafanyika siku moja kabla ya siku ya upigaji kura au siku nyingine yoyote kama itakavyoamuliwa na Tume.

“Upigaji kura wa mapema chini ya kifungu kidogo cha (1) cha kifungu hiki utatumika katika uchaguzi mkuu au uchaguzi mdogo wa urais pekee,” imeeleza sheria hiyo.

Makundi mengine yaliyotajwa katika sheria hiyo ni wasimamizi wa uchaguzi wa wilaya, wasaidizi wasimamizi wa majimbo, watendaji wa vituo ambao watasimamia vituo siku ya uchaguzi, askari polisi waliopangiwa majukumu siku ya uchaguzi na mpigakura yeyote ambaye amepangiwa dhamana ya ulinzi siku ya uchaguzi.

Sheria hiyo inaruhusu kura ya mapema kwa wananchi wa Zanzibar ili kutoa nafasi ya kupiga kura kwa watu ambao kutokana na majukumu ya kusimamia uchaguzi wanakosa nafasi ya kupiga kura kwani sheria inamtaka mwananchi kupiga kura mahali alipojiandikisha.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Uchaguzi INEC, Ramadhani Kailima alisema katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu wapigakura 37,647,235 wameandikishwa Tanzania Bara na Tanzania Zanzibar.

Kailima alisema kati ya wapigakura 37,647,235, wapigakura 36,650,932 wapo Tanzania Bara na wengine 996,303 wapo Tanzania Zanzibar.

Katika Daftari la Wapigakura la Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) wameandikishwa wapigakura 717,557.

“Daftari la Wapigakura la Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar litakuwa ni sehemu ya Daftari la Wapigakura la Tume ya Huru ya Taifa ya Uchaguzi kwa ajili ya uchaguzi wa rais na wabunge upande wa Tanzania Zanzibar,” alieleza.

Habari Zifananazo

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Back to top button